Kumekucha Kombe la Mtaa kwa Mtaa Lindi

Muktasari:

Mashindano ya Mtaa kwa Mtaa Cup 2019, yatasaidia ujenzi wa kituo cha kutolea elimu ya lugha ya alama kwa mkoa wa Lindi.

Lindi. Mashindano ya Kombe la Mtaa Kwa Mtaa yameanza kutimua vumbi mkoani Lindi na kushirikisha timu 20 za kutoka Manispaa hiyo kauli mbiu isemayo ‘vumbua na thamini vipaji’.

Mashindano hayo yamezinduliwa juzi Jumapili na makamu wa Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) Athuman Nyamlani kwenye Uwanja wa Mpilipili, Lindi Mjini.

Mratibu wa mashindano hayo Prosper Kulita alisema lengo la mashindano ya Mtaa kwa Mtaa ni kuirudishia jamii kwa kutambua na kuthamini vipaji vya wachezaji wachanga.

Kulita alisema mashindano ya Mtaa kwa Mtaa Cup 2019, yatasaidia ujenzi wa kituo cha kutolea elimu ya lugha ya alama kwa mkoa wa Lindi.

Timu 20 zinazoshiriki mashindano hayo ni pamoja na Bingwa mtetezi Lukuti FC, Black Tiger FC, Lindi Soccer Academy, Mtanda FC, Bodaboda FC, Msufini FC, Wachukuzi FC, Likotwa FC, Muhimbili FC, Msinjahili FC, Mkuraba FC, Raha Leo FC, Chinowa Academy, Beach Place FC, Angola FC, Madogo Soka, Madigidi FC, Brigita FC, Carrie cops FC.

Mashindano hayo yanatarajia kufanyika kwa mtindo wa mtoano kwa awamu ya kwanza ambapo timu 12 zitaingia katika makundi kufuzu hatua ya robo fainali, na hatimaye nusu fainali na fainali.

Baada ya kukamilika katika Manispaa ya Lindi mashindano haya yatachezwa pia katika wilaya zote za mkoa wa Lindi kuanzia Liwale, Nachingwea, Kilwa na Ruangwa ili kupata washindi wawili kila wilaya ambao watashiriki mashindano ya mkoa ambayo yataitwa (Super 8) yanayoshirikisha timu nane kwa mkoa mzima.

Mshindi wa jumla katika Ligi ya mkoa (Super 8) anatarajia kupata zawadi ya Gari na mshindi wa pili zawadi ya Pikipiki.