Lukaku awapa raha Chelsea
CHELSEA imeanza harakati za kulitetea taji lao la Ligi ya Mabingwa Ulaya kwa ushindi wa bao 1-0 lililofungwa na Romelu Lukaku dhidi ya Zenit St Petersburg.
Lukaku, ambaye alisajiliwa kwa Pauni 97.5milion akitokea Inter Milan, ameonekana kuwa mwarobaini wa kocha Thomas Tuchel kwenye safu yake ya ushambuliaji.
Katika mchezo huo ambao vijana wa Tuchel walikuwa nyumbani kwenye uwanja wao wa Stamford Bridge, iliwabidi kusubiri hadi dakika 69 kupata bao lililofungwa kwa kichwa na Lukaku na yote hiyo ilitokana na upinzani ambao Zenit St Petersburg ilikuwa ikiuonyesha.
Haukuwa mchezo mwepesi kwa Chelsea kwani Zenit walionekana kuwa na mbinu madhubuti ambazo ziliwanyima uhuru matajiri hao wa London ambacho licha ya kumiliki mchezo huo kwa kiwango kikubwa lakini hawakuonekana kuwa na madhara.
Zenit walionekana kuziba mianya ya mashambulizi kwa Chelsea huku wakijenga mashambulizi yao kwa kustukiza hilo lilionekana kufanya kazi kwao kutokana na kikosi chao kuundwa na wachezaji wenye kasi hivyo ilikuwa rahisi kwao kutekeleza mipango yao.
Hata hivyo uzoefu wa wababe hao wa London na ubora wa kikosi chao uliwabeba na kupata bao hilo ambalo lilikuwa la nne kwa Lukaku kwenye mashindano yote tangu ajiunge na klabu hiyo huku likiwala kwanza kwenye ligi hiyo ya mabingwa Ulaya.
Karata ya pili kwa Chelsea kwenye hatua hiyo ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya itakuwa, Septemba 29 huko Italia dhidi ya Juventus ambao kwenye mchezo wa kwanza waliitandika Malmo dozi ya mabao 3-0.