Kocha afurahi Hojlund, Amad kugombana
Muktasari:
- Hojlund alitokea benchini kwenye mechi hiyo na kufunga mara mbili akiipa Man United ushindi wao wa kwanza ugenini kwenye michuano ya Ulaya tangu Machi 2023, wakiweka hai matumaini yao ya kutinga hatua mtoano moja kwa moja bila ya kusubiri mechi za mchujo.
MANCHESTER, ENGLAND: KOCHA, Ruben Amorim amemshuhudia straika wake matata Rasmus Hojlund akilumbana na mchezaji mwenzake wa Manchester United, Amad baada ya mechi ya Viktoria Plzen na kuwataka waendelee kulumbana kwani ni afya kwenye timu.
Hojlund alitokea benchini kwenye mechi hiyo na kufunga mara mbili akiipa Man United ushindi wao wa kwanza ugenini kwenye michuano ya Ulaya tangu Machi 2023, wakiweka hai matumaini yao ya kutinga hatua mtoano moja kwa moja bila ya kusubiri mechi za mchujo.
Lakini, Hojlund na Amad walionekana kupishana lugha baada ya filimbi ya mwisho wakilaumiana baada ya kunyimana pasi kwenye mashambulizi mawili ya kushtukiza waliyofanyia kwenye dakika za majeruhi.
Badala ya kuchukizwa na jambo hilo, kocha Amorim alisema anakaribisha malumbano kama hayo kwa wachezaji wake kwa sababu yanakuwa yamebeba dhamira ya kutaka timu ifanye vizuri, aliposema: “Kwangu mimi ile ni safi.”
Amorim aliongeza: “Tunataka tuwe na hisia fulani. Katika kipindi kama hilo, tunahitaji kuwa na hisia. Kama tunataka kupambana wenyewe kwa wenyewe kama kwenye familia, hiyo ni dalili nzuri sana. Tunataka tuone ule uchungu na hilo ni jambo muhimu kwa timu.”