Chelsea ikubali tu yaishe

MANCHESTER, ENGLAND. MANCHESTER United inatarajia kutuma pesa ofa ya mwisho yenye thamani ya Pauni 55 milioni kwaajili ya kiungo Mason Mount.
Hiyo ni baada baada ya ofa yao ya pili ya Pauni 45 milioni pamoja na nyongeza ya Pauni 5 milioni kukataliwa na The Blues.
Kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na Fabrizio Romano, kocha Erik ten Hag anadhani kiwango hicho cha pesa ni kubwa, na endapo watashindwa kufikia makubaliano watajiondoa kwenye mbio za kuwania saini yake
Vilevile Man United wako tayari kujiondoa kwenye mazungumzo ikiwa ofa hiyo mpya haitakubaliwa, na watasaka kiungo mwingine.
Mount, ambaye ameichezea The Blues mechi 200, alichaguliwa kuwa Mchezaji bora wa mwaka wa Chelsea kuanzia msimu wa 2020-21 na 2021-22, lakini sasa imeonekana wazi hana mpango wa kukipiga Stamford Bridge msimu ujao.
Mount aliisaidia Chelsea kubeba ubingwa wa Ligi Mabingwa Ulaya mwaka wa 2021, alifunga mara mbili dhidi ya Porto na Real Madrid kwenye mechi ya robo fainali.
Kiwango cha mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 24 kimetatizwa na majeraha ya mara kwa mara msimu uliopita, na akafanyiwa upasuaji wa goti.
Chelsea ilijaribu kufanya mazungumzo ya mkataba mpya na Mount, Februari mwaka huu lakini hawakufikia makubaliano kwenye mshahara.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Uingereza ni mmoja ya kiungo ambaye ataondoka kwenye dirisha hili la usajili la kiangazi na atataka akipige Man United msimu ujao.