Straika matata atua Simba

Straika wa Burundi, Laudit Mavugo
Muktasari:
Straika huyo anatua jijini Dar es Salaam leo Jumamosi kwa ajili mazungumzo na Simba kabla ya kusaini kukipiga katika timu hiyo kwa msimu ujao wa Ligi Kuu Bara.
WAKATI wakiendelea kufanya mchakato wa kumleta kocha wa makipa wa AFC Leopards, Abdul Idd Salim, aliyewahi kumnoa Ivo Mapunda akiwa Gor Mahia, Simba imemwita rasmi nchini straika wa Burundi, Laudit Mavugo.
Straika huyo anatua jijini Dar es Salaam leo Jumamosi kwa ajili mazungumzo na Simba kabla ya kusaini kukipiga katika timu hiyo kwa msimu ujao wa Ligi Kuu Bara.
Vigogo wa Simba walianza kufanya mazungumzo ya awali na straika huyo ambapo juzi kigogo mmoja wa Wekundu hao ambaye yupo katika Kamati ya Mashindano aliamua kumpandia ndege kwa ajili ya kumleta nchini.
Inaelezwa mchongo mzima wa usajili wa mchezaji huo ukiunganishwa na mshambuliaji wa zamani wa Simba, Suleiman Ndikumana.
Endapo Mavugo atakubaliana na viongozi wa Simba kusaini mkataba, basi atafikisha idadi ya wachezaji watano wa kigeni baada ya Emmanuel Okwi, Juuko Murshid na Simon Sserunkuma ambao wote ni raia wa Uganda na Raphael Kiongera raia wa Kenya anayecheza kwa mkopo katika klabu ya KCB ya kwao.
Simba imedokeza kwa sasa imebakiza nafasi tatu za kuziba kabla ya kufunga usajili wake, wachezaji inaowataka ni kipa mmoja, straika na beki wa pembeni, majina ya nafasi zote hizo yameshapendekezwa.
Baaadhi ya mapendekezo hayo ni Malimi Busungu, Emery Basiyenge, Mavugo na David Mwantika.
Simba imefanikiwa kuwanasa Mohamed Faki, Samih Haji Nuhu, Mussa Hassan ‘Mgosi’ ambaye amewahi kuichezea timu hiyo na Peter Mwalyanzi huku Said Ndemla, Ibrahim Ajibu na Hassan Isihaka wakiongezwa mikataba mipya.