Nyota Savio aongoza kutupia BDL

Muktasari:
- Mchezaji huyo amegeuka moto katika mashindano hayo na ubora wake umekuwa ukionekana kila anapokuwa karibu na nyavu, kwani ni nadra kukosa kikapu anaposhuti.
WAKATI ushindani wa ufungaji ukiendelea katika Ligi ya Kikapu Mkoa wa Dar es Salaam (BDL), huko kunaonyesha kwamba nyota wa Savio, Ntibomela Bukenge ndiye anayeongoza kwa ufungaji akiwa keshatupia pointi 124.
Mchezaji huyo amegeuka moto katika mashindano hayo na ubora wake umekuwa ukionekana kila anapokuwa karibu na nyavu, kwani ni nadra kukosa kikapu anaposhuti.
Bukenge katika mashindano hayo anafuatiwa na Enerico Maengela wa ABC aliyefunga pointi 118, Jamel Marbuary (Dar City 106), Jonas Mushi (Stein Warriors 100) na Jamal Hussein wa Mchenga Stars aliyetupia pointi 91.
Akizungumzia ligi ya kutupia nyavuni, Kamishina wa Ufundi na Mashindano wa BDL, Haleluya Kavalambi alisema imekuwa ya moto ya inaonyesha kwamba ligi hiyo msimu huu imeongezeka ubora wake.
Kwa mujibu Kavalambi, kwa upande wa ufungaji wa eneo la mtupo mmoja wa three points anayeongoza ni Peter Chacha wa Mchenga Stars aliyefunga 17 akifuatiwa na Zadock Emmanuel (Kurasini Heat) aliyetupia 16, huku Mikado Ebengo (UDSM Outsiders) akifanya hivyo mara 14, Jamel Marbuary (Dar City 14) na Jonas Mushi (Stein Warriors 13).
Kwa upande wa asisti kuna Alinani Msongole wa ABC anayeongoza kwa kutoa 33 akifuatiwa na Omary Sadick (JKT 29), Amin Mkosa (Dar City) na Said Mlowa (Kurasini Heat) 24 kila mmoja huku Gideon Barnabas wa Mgulani JKT akiwa nazo 23.
Katika ribaundi anayeongoza ni Lawi Mwambasi wa Polisi Stars aliyedaka mipira mara 60 akifuatiwa na Elias Nshishi (ABC 59), Aloyce Boniface (Mchenga Star 56), Daniel Damas (Mchenga Stars 52) na Soro Godfrey wa Pazi 49 huku Englbert Machumu wa KIUT akiongoza kuzuia mipira (block) mara 13 akifuatiwa na Fotius Ngaiza (Vijana ‘City Bulls’ 9), Kanyimba Dani (UDSM 8) na Jordan David wa JKT mara 8.

WANATAJWA SANA
Katika ligi hiyo hutakosa kuyasikia majina ya wachezaji yakitajwa tajwa ya Oswald Bera (DB Oratory), Juliana Sambwe (Tausi Royals) na Jesca Lenga (DB Troncatti) ambao wanacheza kama namba moja (point guard) kutokana na kuwa vivutio.
Nafasi ya point guard imebeba jukumu la kupokea mipira yote inayoanza na kupeleka upande wa pili kwa ajili ya mashambulizi na hao wanaonekana kuwa na uwezo mikubwa kutokana na uwezo kutumikia vizuri nafasi hiyo pamoja na kufunga.
Bera ambaye ni raia DR Congo, mbali ya kuiunganisha vyemaa DB Oratory, pia ni mchezaji mwenye uwezo mkubwa wa kutoa asisti na kufunga katika maeneo yote ya uwanja, huku Juliana mbali ya kucheza vizuri namba 1 ana uwezo pia wa kudaka mipira ya ribaundi, kufunga, kutoa asisti na kupokonya (steal).
Kwa upande wa Jesca, mbali ya kuunganisha timu yake vizuri sifa aliyonayo nyingine ni uwezo wa kupenya katikati ya walinzi bila kuguswa na kutoa asisti sambamba na kufunga.

POLISI YAITIA KOROKONI PAZI
Polisi Stars iliinyuka Pazi Queens kwa pointi 55-44 katika Ligi ya Kikapu Mkoa wa Dar es Salaam (WBDL) kwenye Uwanja Donbosco, Upanga ikiuanza mchezo katika robo ya kwanza na kumaliza ikiwa mbele kwa pointi 15-1, huku robo ya pili Pazi Queens ilijibu kwa pointi 23-17.
Katika robo ya tatu Pazi Queens iliongoza tena kwa pointi 14-13 na ile ya nne Polisi Stars ikapata pointi 10-6.
Katika mchezo huo Irene Kapambala alifunga pointi 24 akifuatiwa na Makerenge Hassan aliyefunga pointi 10, huku upande wa Pazi Queens alikuwa Maria Mbena aliyefunga pointi 20 akifuatiwa na Maria Kapambala aliyefunga pointi 10.

SRELIO HOI KWA ORATORY
Kujiamini kwa Srelio dhidi ya DB Oratory katika BDL kuliifanya ichezee kichapo cha pointi 76-72, ambapo Srelio ilianza mchezo taratibu na kuifanya ifike kila mara katika eneo la wapinzani wao.
Hata hivyo, DB Oratory ilitumia nafasi hiyo kufunga pointi 22-14 katika robo ya kwanza kwa kutumia vyema nafasi ilizozipata tofauti na Srelio ambao kila walipofika eneo hilo waliishia kupoteza mipira.
Kujiamini huko kwa Srelio kuliipa nafasi DB Oratory kuonyesha ubora, jambo lililofanya iongoze tena kwa pointi 27-17 huku robo ya tatu Srelio ikiziduka na kuongoza kwa pointi 19-15 na ya nne ikavuna 22-12.
Katika mchezo huo Isaya William aliongoza kwa kufunga pointi 24 akifuatiwa na Hassan Kabanda aliyetupia 23, huku upande wa Srelio alikuwa ni Lerry Mve aliyefunga pointi 22 akifuatiwa na Dan Kola aliyeweka nyavuni 21.