Ngorongoro Heroes yatolewa Afcon, Kocha ajitetea

KOCHA Mkuu wa Ngorongoro Heroes Jamhuri Kihwelo Julio, amesema licha ya kuondoshwa katika michuano ya Afcon U-20 vijana wake wamejifunza vitu vingi vitakavyowasaidia mbeleni.
Ngorongoro ilipangwa Kundi C katika michuano hiyo inayoendelea kutimua vumbi nchini Mauritania ikiwa na timu ya Gambia ambayo walitoka sare ya bao 1-1, wakifungwa mabao 4-0 na Ghana na jana kufungwa na Morocco mabao 3-0.


Julio amesema michuano hiyo imempa kitu cha kujifunza kama mwalimu ambacho kitawasaidia katika michuano ijayo.
"Mashindano ni mazuri, tumepoteza ni sehemu ya mchezo ila nina imani vijana wangu wamepata vitu ambavyo vitatusaidia mbeleni," anasema Julio.
Julio amesema kila timu katika michuano hiyo imejipanga na hata wao walijipanga lakini bahati haijawa upande wa Tanzania.
Ngorongoro imejitupa dimbani mara tatu ikikubali mabao nane huku wenyewe wakiambulia kufunga bao moja pekee.