Nabi awawekea mtego Djuma, Moloko

Muktasari:

Beki Djuma Shaban na kiungo mshambuliaji Jesus Moloko walipewa ruhusa ya siku saba wakirejea kwao nchini DR Congo kushughulikia pasi zao za kusafiria ambapo wamerejea jana ndani ya muda waliopewa.

Wakati Yanga ikibakiza saa chache kushuka Uwanja wa Mkapa kujipima dhidi ya JKU ya Zanzibar kocha mkuu wa timu hiyo Nesreddine Nabi anapanga kuwawekea mtego mastaa wake wawili wa kigeni beki Djuma Shaban na kiungo mshambuliaji Jesus Moloko.

Nabi amesema anafikiria kuwapa muda wa kucheza wachezaji hao wawili katika mchezo huo ukiwa ni kipimo kama walitekeleza ipasavyo programu maalum ya mazoezi aliyowapatia kabla ya kuondoka.

Djuma na Moloko walipewa ruhusa ya siku saba wakirejea kwao nchini DR Congo kushughulikia pasi zao za kusafiria ambapo wamerejea jana mchana na moja kwa moja wamejiunga na kambi ya timu hiyo.

Nabi amesema endapo atagundua mapungufu kwa wachezaji hao wawili kwa kutofuata vizuri programu hiyo watakumbana na rungu la adhabu.

"Wamerudi ndiyo Djuma na Jesus tuko nao waliondoka nna kuna programu maalum tuliwapa nafikiria kuwapa nafasi katika mchezo wa baadaye,"amesema Nabi.

"Tukiona kama hawakufanya kile tulichowaelekeza watapata adhabu watakuwa wamejitofautisha kwa nafasi kubwa na wenzao ambao walibaki.

"Sina tatizo sana na hawa ambao wamekwenda timu za taifa naamini watakuwa wanafanya mazoezi makali kuna kitu kitakuwa kipo sawa kwao."

Aidha Nabi amesema katika muda ambao ligi imesimama wamekuwa katika muda mzuri wa kufanya mazoezi makali kwa siku mara mbili ambayo yameongeza ubora wao na sasa wanataka kupima kil;e ambacho wamekifanya katika mchezo wa leo.