Mtanzania kusaka viwango vya michezo ya Madola Afrika Kusini

Muktasari:
- Sauda mbali na kusaka nafasi ya Madola, alikuwa miongoni mwa wanamichezo wawili wa Paralimpiki waliofuzu, kuiwakilisha nchi kwenye Olimpiki ya msimu uliokwisha nchini Japan.
Mwanariadha wa paralimpiki, Sauda Njopeka amepata nafasi ya kushiriki mafunzo na mashindano ya kutafuta viwango vya kushiriki michezo ya Jumuiya ya Madola.
Sauda ataondoka nchini keshokutwa Alhamisi sanjari na kocha mkuu wa timu ya taifa ya Paralimpiki, Bahati Mgunda kwenda Afrika Kusini tayari kwa mafunzo na mashindano hayo yatakayofanyika kwa siku tano kuanzia Ijumaa.
Katika mafunzo na mashindano hayo ambayo ni ya programu ya Gaps yanayoshirikisha wanamichezo wenye ulemavu, Sauda ni Mtanzania pekee aliyepata nafasi hiyo.
"Kama atafanya vizuri, atafuzu kushiriki michezo ijayo ya Madola," amesema Henry Tandau, makamu mwenyekiti wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC).
Amesema katika michezo ya Madola, Paralimpiki pia inaratibiwa na TOC tofauti na ilivyo kwenye Olimpiki ambayo michezo hiyo inaratibiwa na Kamati ya Paralimpiki.
"Kwenye michezo ya walemavu kuna tofauti ya ushiriki msimu huu wa Madola, wanatakiwa kufikia viwango, hivyo Sauda kama atafanya vizuri Afrika Kusini ataungana na wawakilishi wengine wa Tanzania kwenye michezo hiyo baadae Julai nchini Uingereza," amesema.
Michezo mingine itakayoiwakilisha nchi ni riadha, judo, ngumi na kuogelea.
Kocha Mgunda amesema kutokana na rekodi ya mchezaji huyo, wana matumaini makubwa ya kufuzu.
"Sauda yuko kwenye daraja la tano T57, nchini Afrika Kusini atachuana kwenye kutupa tufe lakini pia tumepewa nafasi kwenye kisahani na amekuwa akijifua katika michezo hiyo miwili ya mitupo," amesema Mgunda wakati wa kukabidhiwa tiketi na posho kutoka Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC) ambayo imesapoti ushiriki wa Tanzania.
Wawakilishi hao Watanzania wataondoka keshokutwa kupitia Addis Ababa, Ethiopia na kisha kuelekea Afrika Kusini ambako kutakuwa na mafunzo na mashindano ya Paralimpiki kwa siku tano kuanzia keshokutwa.
Rais wa TOC, Gulam Rashid, Tandau, Katibu mkuu, Filbert Bayi na naibu katibu mkuu, Suleiman Jabir waliwatakia safari njema Sauda na kocha wake, huku Gulam akisisitiza kuitumia vema nafasi hiyo.
"Ni nafasi ya pekee kwao na kati ya nchi 72 zilizo kwenye michezo ya Madola, Tanzania tumekuwa miongoni mwa nchi 15 tulizopata fursa hiyo," amesema Gulam na kuongeza.
"Pia mchezo wa kunyanyua vitu vizito umeingia kwenye programu hii na safari ya mchezaji na kocha imeanza kuraratibiwa wao wataondoka karibuni kwenda Uingereza kwenye mafunzo hayo," amesema.
Amesema TOC imesapoti usafiri na posho dola 975 kwa kila mmoja kwenye msafara huo kwa ajili ya matumizi yao watakapokuwa kwenye mafunzo hayo.