Morocco amtanguliza Bigirimana wakiwafuata Yanga

Muktasari:
Mchezo huo utakuwa ni dakika 90 za kwanza kwa kocha mpya wa Namungo FC Hemed Morocco wakiwa wageni wa Yanga ambapo kocha huyo amepewa ajira hiyo kuchukua nafasi ya Mrundi Thiery Hitimana ambaye alitimuliwa wiki hii.
Kocha mpya wa Namungo FC Hemed Morocco amemtanguliza mbele mshambuliaji Bigirimana Blaise wakati kikosi chake kikiwa wageni wa Yanga katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Morocco mchezo huo unakuwa wa kwanza kwake tangu apewe ajira hiyo akichukua nafasi ya Thiery Hitimana ambaye alitimuliwa mapema wiki hii na uongozi wa klabu hiyo.
Katika safu ya ulinzi Morocco amewaanzisha kipa Mrundi Jonathan Nahimana wakati beku wa kulia akiwa Miza Kristom,kushoto akicheza Edward Manyama wakati mabeki wa kati wakiwa Kalos Protas na nahodha wake Hamis Mgunya.
Namungo ambao watakuwa wakitumia mfumo wa 4-2-3-1 katika kiungo wataanza na Fredy Tangalo na Hamis Khalifa wataocheza kiungo cha chini.
Juu yao watakuwa Sixtus Sabilo kiungo mchezeshaji Lucas Kikoti sambamba na kiungo mshambuliaji Stephen Sey huku safu ya ushambuliaji Bigirimana Blaise akitangulizwa peke yake.
Kwenye benchi Morocco amewapa nafasi kipa Lucas Chembeja mabeki wakiwa Haruna Shamte,Jafary Mohamed ,Frank Magingi viungo wakiwa Idd Kipagwile,Shiza Kichuya na mshambuliaji Adam Salamba.
Na KHATIMU NAHEKA