Morice amkosha kocha wake

MCHEZAJI kinda wa Tanzania, Morice Abraham, 18, ambaye anacheza soka la kulipwa nchini Serbia kwenye klabu ya Spartak Subotica ameonakana kumkosha kocha wake, Vladimir Gacinovic kiasi cha kuahidiwa kuendelea kupewa nafasi kwenye kikosi.
Tangu amejiunga na Spartak Subotica, Julai mosi, mwaka huu, licha ya kuwa na umri mdogo, Morice amefanya makubwa kwenye kikosi hicho ambacho kinashiriki Ligi Kuu nchini humo ambayo ni maarufu kama Serbian Super Liga.
Katika moja ya mahojiano yake ambayo alifanya hivi karibuni, Vladimir ambaye alimpanga Morice kwenye mchezo dhidi ya Red Star Belgrade, alisema anavutiwa na uchezaji wa kinda huyo hivyo ni wajibu wake kuhakikisha anakiendeleza kipaji chake.
“(Morice) ni mchezaji mzuri na mwenye kipaji cha aina yake. Binafsi nimekuwa nikivutiwa na uchezaji wake, anaonyesha kuwa na shauku ya kucheza. Ni jambo zuri na jema tutaendelea kumpa nafasi taratibu kulingana na mahitaji ya timu,” alisema kocha huyo.
Katika mchezo wa ligi dhidi ya Red Star Belgrade, Morice alicheza kwa dakika 52.
Vladimir alimpa nafasi kinda huyo ya kuanza kwenye kikosi chake cha kwanza ambapo Spartak Subotica walitandikwa kwenye mchezo huo kwa mabao 3-0 wakiwa ugenini.
Morice ambaye ni miongoni mwa wachezaji wa Tanzania wenye ndoto kubwa ya kuipeperusha vyema bendera ya nchi kwenye moja ya ligi kubwa zaidi duniani, aliwahi kusema kuwa Serbia kwake amepanga kupatumia kama njia ya kufikia malengo yake.
“Malengo yangu ni makubwa. Naamini Mungu atanisaidia ili kuyatimiza. Natamani kucheza soka kwenye ligi kubwa zaidi kama ambavyo ametuonyesha njia kaka yetu Samatta,” alisema.
Morice amekuwa na uhusiano wa karibu na Samatta na mara kadhaa wamekuwa wakionekana kuwa pamoja sambamba na Kelvin John ambaye anakipiga kwenye timu ya vijana ya KRC Genk nchini Ubelgiji.