Mingange aahidi makubwa Lipuli

Dar es Salaam. Kocha wa Lipuli FC, Abdul Mingange amesema baada ya kuanza vyema kwenye mchezo wa kwanza wa Ligi Daraja la Kwanza (FDL) imewapa nguvu ya kuzidi kupambana.

Mingange alisema timu yoyote inakuwa na uhakika wa kupata ushindi kwenye mchezo kutokana na maandalizi bora ya kuwakabili wapinzani wake.

“Timu yangu ipo vizuri na wikiendi hii nakutana na Gipco FC, nisema ukweli siwajui vizuri na wala sijawahi kuwaona, lakini naamini vijana wangu watapambana vilivyo.

“Jana (juzi) tulicheza na Mbeya City mchezo wa kirafiki na leo (jana) tumecheza na Iringa Combine ili kuzidi kuwaweka fiti wachezaji,” alisema.

Mingange aliongeza kuwa anajivunia kuwa na wachezaji wazuri kutokana na kulitumia vyema dirisha la usajili kwa kupata wachezaji walio bora.

Lipuli FC ilianza ligi kwa kuichapa Mawenzi Market mabao 2-1 yaliyofungwa na Shaban William na Bonface Maganga huku lile la kufutia machozi kwa Mawezi likifungwa na Johnson Clement.

Lipuli itaondoka Iringa kesho kwenda Mbeya kukipiga na Gipco FC, ambayo ilianza ligi kwa kulala bao 1-0 dhidi ya Boma FC.