Mazembe yaiweka Simba mtegoni

Muktasari:

  • Tishio hilo linaloiweka Simba kwenye mtego huo wa kuporomoka kwenye viwango unachangiwa zaidi na TP Mazembe ya DR Congo iliyofuzu nusu fainali ya msimu huu kwa kuing'oa Petro Atletico ya Angola, lakini kukiwa pia na timu nyingine tatu zilizopo Kombe la Shirikisho Afrika.

SIKU chache tangu itolewe katika hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika, Wekundu wa Msimbazi, Simba inanyemelewa na pigo lingine ambalo ni kushuka kwa nafasi tatu kwenye viwango vya ubora vya Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kwa msimu ujao wa 2024/2025.

Tishio hilo linaloiweka Simba kwenye mtego huo wa kuporomoka kwenye viwango unachangiwa zaidi na TP Mazembe ya DR Congo iliyofuzu nusu fainali ya msimu huu kwa kuing'oa Petro Atletico ya Angola, lakini kukiwa pia na timu nyingine tatu zilizopo Kombe la Shirikisho Afrika.

Kwa sasa, Simba ipo katika nafasi ya tano katika viwango vya ubora vya klabu vya CAF ambavyo vimepatikana kwa kujumlisha alama ambazo timu zimekusanya katika mashindano ya Ligi ya Mabingwa na Kombe la Shirikisho Afrika ambayo yako chini ya usimamizi wa shirikisho hilo la soka la Afrika.

Simba ipo katika nafasi hiyo ya tano ikiwa imekusanya pointi 39, nyuma ya kinara Al Ahly iliyo na pointi 77 hadi sasa, Wydad yenye pointi 60, Esperance na pointi zake 56 huku Mamelodi Sundowns ambayo ina pointi 54.

Lakini wakati Simba sasa ikiwa nje ya mashindano ya klabu ya CAF, zipo timu nne ambazo haijazipita kwa idadi kubwa ya pointi ambazo bado zinashiriki mashindano hayo msimu huu na kama zitafanya vizuri katika hatua zilizopo, basi Simba itajikuta ikiporomoka hadi nafasi ya tisa kutoka ile ya tano iliyopo sasa.

Timu hizo ambazo zinahatarisha nafasi ya tano ya Simba kwenye viwango vya ubora vya Klabu vya CAF kwa kutazama mafanikio ya misimu mitano iliyopita ni TP Mazembe ya DR Congo, Zamalek  (Misri), USM Alger (Algeria) na RS Berkane ya Morocco.

TP Mazembe iko nafasi ya saba ikiwa na pointi 38 na kama itafanikiwa kuitupa nje Al Ahly na kutinga katika hatua ya fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika, itakaa katika nafasi ya tano ambayo Simba ipo hivi sasa kwa vile timu hiyo ya DR Congo itakuwa imefikisha pointi 43.

Zamalek ambayo iko nyuma ya TP Mazembe ikiwa nafasi ya nane na pointi 38, ipo katika hatua ya nusu fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika ambapo itakutana na Dreams ya Ghana ambapo ikipenya na kuingia fainali, itafikisha pointi 42 kutoka 38 ilizonazo sasa.

RS Berkane kwa sasa ina pointi 37 na kama itaitoa USM Alger na kutinga fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika itafikisha pointi 41 ambazo zitazidi kuidondosha Simba.

KImahesabi ni kwamba ikiwa Berkane itatolewa, bado Simba haitokuwa katika nafuu kwani USM Alger itaitoa mahali ilipo kwa vile timu hiyo ya Algeria itafikisha pointi 41 kwani kwa sasa ina pointi 36.

Pointi za timu hizo zinaweza kuwa zaidi ya hizo ikiwa mojawapo au mbili zitafanikiwa kutwaa ubingwa katika mashindano ambayo inashiriki.

Faida ya kuwemo katika nafasi ya tano ni kuifanya timu iwekwe katika chungu namba moja au mbili katika droo ya hatua ya makundi ya mashindano ya klabu ya CAF ambapo inapata fursa ya kutopangwa dhidi ya timu nyingi ngumu, bora na zenye uzoefu.

Lakini, faida nyingine ni kuanzia katika hatua ya kwanza ya mashindano ya klabu Afrika iwapi kunakuwa na timu zimeamua kutoshiriki mashindano hayo.

Kwa misimu karibu minne mfululizo kwa sasa Tanzania imekuwa ikitoa timu nne katika michuano ya CADF, mbili zikicheza Ligi ya Mabingwa na nyingine katika Kombe la Shirikisho ambalo Yanga ilifuika fainali msimu uliopita na kupoteza kwa kanuni ya bao la ugenini mbele ya USM Alger baada ya matokeo ya jumla kuwa sare ya 2-2, Yanga ikilala nyumbani 2-1 na kushinda ugenini kwa bao 1-0.