Jamaa kaipania Simba kinoma leo kwa Mkapa

KOCHA Mkuu wa Mtibwa Sugar, Salum Mayanga amesema amewafanyia tathimini wapinzani wake Simba wakati timu hizo zinapokutana leo saa 1 usiku kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa katika mchezo wa duru ya pili mzunguko wa 28.

Akizungumza Jijini Dar es Salaam jana, Mayanga alisema licha ya kiwango bora cha Simba kwenye michezo miwili iliyopita ila hilo haliwapi hofu kwani amejiandaa kukabiliana nao na kuhakikisha hawapi nafasi.

“Wana wachezaji wazuri ambao wanaweza kuamua mechi hivyo tumezingatia yote hayo kwa maana ya kuziba mianya pindi wanapotushambulia kwani wanaonekana wakiwa bora wakipitia pembeni,” alisema na kuongeza;

“Hatuwezi kucheza na mchezaji mmoja bali kama timu nzima, hii itatusaidia sana kuwadhibiti na kutowapa nafasi ya kutushambulia mara kwa mara wakati huo sisi tukianzisha mashambulizi yetu kwa kushitukiza.”

Mchezo wa mwisho baina ya timu hizo katika Uwanja wa Benjamin Mkapa, Mtibwa Sugar ilikubali kichapo cha mabao 5-0 Aprili 14, mwaka jana ingawa mzunguko wa kwanza zilitoka suluhu ya 0-0 Januari 22, 2022.

Katika michezo 27, Simba iliyocheza imeshinda 16, sare tisa na kupoteza miwili ikishika nafasi ya pili na pointi 57, huku Mtibwa Sugar ikishinda saba, sare 10 na kupoteza 10 ikishika nafasi ya 12 na pointi 31.