Dabo athibitisha kuwataka Chama, Mzize na Aziz Ki

Muktasari:
- Baada ya kumalizika kwa mechi ya jana ya Azam FC ikiifunga Ihefu bao 1-0 kwenye Uwanja wa Azam Complex, kocha huyo baada ya kuulizwa na wanahabari ni mchezaji gani anaweza akamhitaji kwenye kikosi chake ndipo alipowataja mastaa hao.
Wakati habari za chini ya kapeti zikisema Azam FC inawahitaji mastaa wa Yanga, Stephane Azizi Ki, Clement Mzize, Djigui Diarra na kiungo wa Simba, Clatous Chama kocha wa timu hiyo, Yousuph Dabo, amemwaga mchele.
Baada ya kumalizika kwa mechi ya jana ya Azam FC ikiifunga Ihefu bao 1-0 kwenye Uwanja wa Azam Complex, kocha huyo baada ya kuulizwa na wanahabari ni mchezaji gani anaweza akamhitaji kwenye kikosi chake ndipo alipowataja mastaa hao.
Aliulizwa 'kuna taarifa za Azam kumhitaji Mzize', kocha huyo akajibu: "Hakuna asiyejua uwezo wa Mzize, lakini wapo wengi wazuri kama Chama, Azizi Ki, Diarra na Kibu Denis.
"Sijazungumza na viongozi juu ya hilo, ila ikiwezekana kuwapa basi itakuwa jambo zuri, kwani wanaweza wakaongeza kitu ndani ya kikosi changu.
"Nimewaangalia katika mechi mbalimbali za Ligi Kuu, wameonyesha uwezo mkubwa."
Kwa upande wa msemaji wa timu hiyo, Thabit Zakaria maarufu Zaka za Kazi amesema: "Tupo tayari kumuunga mkono kocha kuhakikisha anapata mahitaji yake, ingawa bado hajaleta hayo majina anayoyataka, isipokuwa Mzize maombi ya kumhitaji yalipelekwa Yanga.
"Uzuri kocha kawataja, wachezaji wengi ambao tunawafuatilia mikataba yao imemalizika, hivyo ni rahisi kuwapata."