Chama, Miquissone wamtisha kocha Al Ahly

Kocha wa Al Ahly ya Misri, Pitso Mosimane amesema amewafuatilia Simba na kubaini ni miongoni mwa timu bora Afrika kutokana na aina yao ya soka ambalo wanacheza.

Mosimane anasema Simba wamenishangaza kushinda mechi ya ugenini dhidi ya As Vita tena Kinshasa mahala ambapo ni pagumu kwa timu pinzani kushinda.

"Katika kuwafuatilia kwangu Simba, nimebaini wana wachezaji wenye uwezo wa kucheza katika kiwango cha juu kwenye mashindano haya makubwa," anasema.

"Miongoni mwa wachezaji hatari wa Simba ambao tunapaswa kuwachunga ni Luis Jose ambaye namfahamu tangu akiwa anacheza soka Afrika Kusini, Chriss Mugalu aliyefunga bao la ushindi ugenini," anasema.

"Wengine MK 14, Meddie Kagere na Mzambia Clatous Chama ambao wote ni wachezaji bora na kesho tutakuwa makini katika kuwazuia na tumejianda katika hilo,"  anasema.

"Simba mechi ya kwanza wamecheza vizuri tena kwa maelewano makubwa, wanacheza soka la kuvutia kwa mashabiki wao, kocha wao namfahamu na nipo na taarifa nyingi dhidi yao huku nikiwa na imani tutashinda," anasema Mosimane.

Nahodha wa Al Ahly, Ayman Ashras anasema wapo tayari kucheza mechi hiyo ambayo wanafahamu itakuwa ngumu.

"Tumekuja kucheza na mabingwa wenzetu katika ligi ya kwao ila tumepanga kukusanya pointi tatu katika mechi hii," anasema.

"Hali ya hewa ya Tanzania ni joto tofauti na ile ya kwetu ila hilo wala halita haribu mipango yetu ya kupata ushindi katika mchezo huu," anasema Ashras.