Aliyetoka Kigoma kwa mguu kuiona Simba atua Dar

HATIMAYE mwanasimba kindakindaki Michael Philibert aliyetoka mkoani Kigoma amefika Jijini Dar es Salaam na kupokelewa kwa shangwe na ndelemo na wanamsimbazi.

Mwamba huyo ametumia siku 15 kutoka Kigoma mpaka Dar es Salaam kwa miguu kwa ajili ya kushuhudia mchezo wa watani wa jadi Simba na Yanga utakaopigwa Julai 3 katika dimba la Benjamin Mkapa.

Ujio wa Michael kwa miguu alipitia mikoa mbalimbali na kupokelewa na mashabiki wa Simba ikiwemo Jijini Dodoma ambako ni makao makuu ya nchi huku Dar es Salaam akipokelewa pia na Mkurugenzi wa Wanachama, Hamisi Kisiwa.

Sio mara ya kwanza kwa shabiki kutoka Kigoma kuja Dar es Salaam kwani Mei 8 shabiki wa Yanga alitoka huko huko huku akiukosa mtanange huo ulioota mbawa baada ya kutokea sintofahamu ya kubadilishwa muda wa mchezo.