Mkude apewa mchongo

KIUNGO Abdallah Seseme wa Kagera Sugar amemuambia mchezaji mwenzake, Jonas Mkude wa Simba bado ana nafasi kubwa ya kuendeleaa kusalia katika kikosi cha kwanza kama anataka.

Seseme na Mkude walishawahi kucheza kwa pamoja katika kikosi cha Simba kabla ya baadae mmoja kuondoka na kwenda kutafuta maisha sehemu nyingine.

Akizungumza na Mwanaspoti, Seseme alisema bado ana imani kubwa na Mkude kutokana na uwezo alionao na ndio maana baada ya kupewa nafasi ameonyesha na anatakiwa aendelee hapo hapo aliposhikilia.

“Mkude ni mchezaji mzuri na alipokuwa hachezi ndio alikuwa na matatizo lakini kwasasa anacheza bila shaka anaonyesha alichonacho,” alisema Seseme.

“Unajua nafasi za kucheza ndio zinakujaga kama hivyo, yeye alikuwa anacheza toka awali na waliokuja walimkuta anacheza, kwahiyo na yeye ni wakati wake wa kushikilia sasa na kufanya vizuri,” alisema Seseme.

Mkude alipoteza nafasi mbele ya viungo Sadio Kanoute na Tadeo Lwanga baada ya kusimamishwa kutokana na utovu wa nidhamu.

Msimu huu baada ya kurejea uwanjani kutokana na majeraha ya Tadeo na Kanoute, Mkude ameonyesha kiwango kizuri.