Warembo 70 Arusha wachuana kumvua taji Miss Tanzania

Muktasari:
Taji la Miss Tanzania linashikiliwa na mrembo, Diana Edward kutoka Kinondoni, linatarajiwa kuanza kuwaniwa Julai sita na warembo kutoka Arusha kabla ya kwenda Dar es Salam kwa ajili ya fainali.
Warembo 70 kutoka sehemu mbali mbali za Jiji la Arusha wanatarajia kuingia kwenye mchujo maalumu wa kusaka taji la mkoa msimu wa mwaka 2018/2019.
Taji la Miss Tanzania linashikiliwa na mrembo, Diana Edward kutoka Kinondoni, linatarajiwa kuanza kuwaniwa Julai sita na warembo kutoka Arusha kabla ya kwenda Dar es Salam kwa ajili ya fainali.
Mratibu wa mashindano hayo, Chilly Kizenga alisema kuwa warembo hao wametoka katika wilaya zote zinazounda Mkoa wa Arusha ikiwemo Arumeru, Karatu, Monduli, Ngorongoro , Longido na Arusha.
"Warembo 70 wameshajiandikisha na wataingia kwenye mchujo kwa kwanza Ijumaa kwa ajili ya kuwapata warembo 20 watakaowania taji la Miss Arusha."
Alisema kuwa mchujo huo utafanyika katika Chuo cha Uandishi wa Habari cha East Afrika eneo la Mianzini kuanzia asubuhi na warembo wote watachujwa na majaji na wasimamizi watakuwepo kuhakikisha kila kitu kinakwenda sawa kumpata mwakilishi aliyetimiza sifa.
"Warembo 20 watakaopatikana Juni moja wataingia kambini kujiandaa na mashindano ya kimkoa yatakayofanyika julai sita katika ukumbi wa AICC jijini Arusha"
Alisema kuwa mshindi wa jumla anatarajiwa kuwakilisha mkoa katika mashindano ya kitaifa yatakayofanyika baadaye jijini Dar es Salaam.