Prime
Yanga yashusha kiungo, yamficha kambini

Muktasari:
- Kiungo huyo mchezeshaji ambaye yupo kambi ya Yanga ni Mohamed Doumbia raia wa Ivory Coast ambaye anaendelea kujifua na wenzake.
YANGA wakati inapiga hesabu za kukutana na Simba, imeendelea na akili ya kukiboresha kikosi na kule kambini kuna mido wa kazi amefichwa akijifua taratibu.
Kiungo huyo mchezeshaji ambaye yupo kambi ya Yanga ni Mohamed Doumbia raia wa Ivory Coast ambaye anaendelea kujifua na wenzake.
Taarifa kutoka Yanga ambazo Mwanaspoti limejiridhisha ni, Doumbia ana wiki moja kwenye kambi ya timu hiyo na taarifa zake hata wachezaji wa timu hiyo wameanza kushtuka juu ya makali yake.
Akiwa mazoezini, Doumbia mwenye umri wa miaka 26 amekuwa hatari kwa kukimbia kwenye nafasi na kupiga pasi za kwenda mbele mithili ya kiungo Mkongomani wa timu hiyo, Maxi Nzengeli.
Mbali na ubora huo, mastaa wa Yanga wamesimulia kiungo huyo ni hatari kwa kupiga mashuti anapokaribia langoni.
Hata hivyo, Yanga bado haijamalizana na kiungo huyo wa kati na eneo la kushambulia ikitaka kujiridhisha zaidi kutokana na kukaa nje kwa takribani miezi mitatu bila timu kuanzia Machi 2025 alipoachana na SC Majestic ya Burkina Faso.
Mbali na SC Majestic, Doumbia anayetumia zaidi mguu wa kulia amecheza soka nchini Jamhuri ya Czech katika timu za Slovan Liberec na Dukla Prague. Pia Ekenäs IF ya Finland.
“Ni mchezaji mzuri kwa mujibu wa taarifa tunazozipata kutoka mazoezini, unajua tulitaka kujiridhisha kwanza ili tusiingie mkenge mwingine wa kumsajili mtu kumbe akawa hana ubora,” alisema bosi mmoja wa juu wa Yanga.
Yanga kuelekea msimu ujao, inasaka kiungo wa eneo la ushambuliaji baada ya kuondoka kwa Stephane Aziz KI ambaye aliitumikia timu hiyo kwa mafanikio makubwa tangu Julai 2022 alipojiunga na timu hiyo akitokea ASEC Mimosas na kuondoka Mei 2025 akitimkia Wydad Casablanca ya Morocco.