Una sifa hizi? unajibebea khadija kopa kiulaiini

Muktasari:
- Kwanza kulikuwa na Khadija Kopa akiwa na kundi lake la TOT Plus huku upande mwingine; Nasma Khamis ‘Kidogo’ na Muungano Dancing Troupe.
KWA wanaokumbuka. Unajua mwanzoni mwa miaka ya 2000, kulikuwa na ushindani mkali katika taarabu iliyokuwa imefifia sana.
Kwanza kulikuwa na Khadija Kopa akiwa na kundi lake la TOT Plus huku upande mwingine; Nasma Khamis ‘Kidogo’ na Muungano Dancing Troupe.
Ilikuwa raha kwelikweli. Sasa ikawa, huku Nasma kule Hadija. Huku kikishushwa kigongo hiki kule kinashushwa hiki, mchezo ukawa uko hivyo. Kwa mapenzi ya Mungu, Nasma kwa sasa yuko mbele za haki.
Hebu tusahau kidogo hayo. Ukimwangalia Khadija Omari Kopa ni mwanamke hasa aliyetimia. Ni mnene wa wastani, rangi yake ni nyeusi yenye mng’ao isiyo hata na tone la carolite au mkorogo. Black beauty babu.
Njoo usoni, umejawa na tabasamu muda wote utadhani hajui kitu kinachoitwa kukasirika.
Licha ya kuwa na umbile hilo, Khadija ni mwepesi wa kunyonganyonga mwili wake atakavyo akiwa stejini akiwa anaimba nyimbo za taarabu, sauti yake nayo ni maridhawa na yenye mvuto wa kipekee.
Wakati mwingine kama inakwaruza kumbe ndio nakshi zenyewe.
Mwanaspoti lilipata kuzungumzia mambo mawili matatu na Khadija Kopa na ilikuwa hivi:
Mwana spoti: Shikamoo Mama.
Khadija Kopa: Marhaba, hujambo?
Mwana spoti: Sijambo. Naomba nifanye mahojiano mawili matatu na wewe juu ya muziki na maisha nje ya muziki.
Khadija Kopa: Hayo mahojiano nje ya muziki yakoje?
Mwanaspoti: Kuhusu maisha halisi mbali na muziki.
Khadija Kopa: Haya niulize, lakini yasiwe ya kudhalilishana.
Mwanaspoti: Wewe ni mwanamuziki wa siku nyingi, unaweza kutaja idadi ya nyimbo ulizoimba hadi sasa?
Khadija Kopa: Kiukweli hata sikumbuki, maana nimeimba nyimbo nyingi sana na nyimbo zingine nilizoimba zamani wala sizikumbuki.
Mwanaspoti: Hadi sasa una miaka mingapi tangu uanze kuimba taarabu?
Khadija Kopa: Nina miaka thelathini na hivi nina mpango wa kufanya onyesho la kutimiza miaka thelathini ya uimbaji baada ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kuisha.
Mwanaspoti: Kuna habari unajihusisha na ushirikina ili upendwe na mashabiki pamoja na nyimbo zako zihit, hii imekaaje?
Khadija Kopa: Hizi habari za ushirikina nimeanza kuambiwa siku nyingi sana, yaani tangu kipindi kile cha upinzaji na Nasma Khamis, hivyo mie nazipuuzia kwani najua kipaji changu ndio kinaniweka juu katika kazi zangu na ndio maana mashabiki wananikubali sana.
Mwanaspoti: Ni kweli tangu Mzee Yusuf aache muziki, taarabu imeyumba?
Khadija Kopa: Aaah wapi! Wala sio kweli, kama Mzee Yusuf kaacha kuimba muziki utayumbaje. Muziki umeanza kuyumba kipindi hata yeye yupo na alikuwa analalamika idadi ya watu wamepungua akipiga pale Travertine.
Tatizo sio Mzee Yusuf kuacha muziki, tatizo ni sisi wenyewe kuufanya muziki kuwa kiingilio bia, nani atakuwa na shauku ya kuuangalia wakati anajua akiingia kununua bia au maji anapata burudani.
Tena mie nasema hii sio kwa muziki wa taarabu tu, bali hata muziki wa dansi tumeuuwa wenyewe sisi wanamuziki kwa kuufanya kuonekana hauna thamani.
Mwanaspoti: Kuna tofauti gani kipindi unaishi na mumeo na sasa uko peke yako?
Khadija Kopa: Utofauti upo, maisha yamekuwa magumu kutokana na kuzoea kuwa na mume wangu karibu na yeye ndio alikuwa msaada mkubwa sana kwangu.
Mwanaspoti: Bado una malengo ya kuolewa tena?
Khadija Kopa: Naolewa ndio! Kwa nini hasa nisiolewe? Tena nataka kuolewa na mwanamume mzee, sitaki kulea watoto wadogo mie.
Mwanaspoti: Ni kweli hujawahi kuchepuka tangu mumeo afariki dunia?
Khadija Kopa: Sijawahi kuchepuka, mchepuko mimi wa nini na umri huu, nina watoto na familia yangu.
Ni kweli mwanamke au mwanamume kuishi pekee yake kwa muda mrefu si sawa, ila huwezi kuchukua mwanamume wa ovyo, kwanza wala sijakulia mazingira hayo, naogopa kuzeeka, kuchoka na kuchuja mapema.
Mwanaspoti: Kitu gani huwezi kusahau maishani mwako?
Khadija Kopa: Kufiwa na mume wangu, yaani sitasahau milele. Alikuwa laaziz haswa. Tajiriba wangu, lakini yote hayo mapenzi ya Mungu.
Mwanaspoti: Pole sana.
Khadija Kopa: Asante.