Mtoto wa Lamata awapatanisha Kajala, Wolper

Muktasari:
- Wawili hao walikutana katika pati hilo lililofanyika Lamata Village na kila mmoja akasema kwa sasa hana kinyongo kutoka moyoni, baada ya kubaini kuwa kuna mwanamume mmoja aliwagombanisha mitandaoni kutokana na kuendekeza mapenzi.
KAMA utani vile, waigizaji nyota wawili wa Bongo Movie, Kajala Masanja na Jacklyne Wolper wamejikuta wakimaliza bifu walilokuwa nalo kutokana na kila mmoja kuwahi kutoka na staa wa Bongo Flava, Harmonize baada ya kukutana katika pati la siku ya kuzaliwa ya mtoto wa Leah Richard ‘Lamata’.
Wawili hao walikutana katika pati hilo lililofanyika Lamata Village na kila mmoja akasema kwa sasa hana kinyongo kutoka moyoni, baada ya kubaini kuwa kuna mwanamume mmoja aliwagombanisha mitandaoni kutokana na kuendekeza mapenzi.
Kwa upande wa Wolper alisema hakuwahi kuwa na ugomvi na Kajala na hata alipoachana na Harmonize, Kajala akaenda kwa Hamornize bado walikuwa ni marafiki ila tu kulikuwa na katabia cha ugombanishi wa watu na yule mwanamume.
“Sijawahi kuwa na shida na Kajala ila watu walihisi kama tumewahi kuwa na shida wakati sisi hizo shida hatujawahi kuziona na watu walianza kusema tuna shida baada ya mimi kuachana na yule bwana, akawa na Kajala hapo ikaanza mambo ya ugombanishi kwa watu na yule mwanamume alikuwa mmoja wao kisa kuendekeza mapenzi,” alisema Jackline Wolper.
Kwa upande wa Kajala alisema, watu hawakuwa wanajua kama yeye na Wolper ni marafiki na hawakuwahi kugombana kama baadhi ya watu wanavyodai, ila tu maneno ya watu mitandaoni ndiyo iliunda maneno na kuonekana wamegombana, hata yule mwanamume alisababisha watu kuwaona wana ugomvi.
“Achana kabisa na hizi biashara dada, sisi tupo katika furaha na hatujawahi kugombana maneno ya mitandaoni ndio yaliunda ugomvi wetu kuwa tuna ugomvi, hata yule mwanamume alisababisha watu kuona tuna ugomvi, sisi ni marafiki sana wa muda mrefu mno,” alisema Kajala.
Mwanaspoti lilipowauliza ni kidume gani wanayemzungumzia, kila mmoja alicheka na kusema kwa heri we hujui wala huogopi.
Katika shughuli hiyo wawili hao walionekana wakiburudika pamoja huku wakicheza kwa pamoja muda wote na walikaa meza moja na walienda kutunza kwa pamoja.
Kwa vipindi tofauti wawili hao waliwahi kutoka kimahaba na Harmonize, akianza Wolper kabla ya Kajala kufuata, japo kila mmoja aliishia kupigwa chini na nyota huyo wa muziki wa kizazi kipya kuhamia kwingine.