Prime
Mondi, Zuchu mambo hadharani

Muktasari:
- Wakati watu wakifuta hesabu za wawili hao kuingia kwenye ndoa ghafla kunaibuka stori za wataoana kisha baadaye mambo yanakuwa tofauti na kuzidi kuongeza hamu ya mashabiki kuona ni kipi kitafuata ili jambo hilo limalizike waendelee na maisha yao. Kwa kifupi, wameanza kuchoka na drama.
KAMA kuna jambo linasubiriwa kwa hamu na mashabiki wa burudani litokee basi ni ndoa ya Diamond Platnumz na Zuhura 'Zuchu', ikiwa ni kapo inayofuatiliwa sana hasa baada ya panda shuka za wawili hao katika mahusiano.
Wakati watu wakifuta hesabu za wawili hao kuingia kwenye ndoa ghafla kunaibuka stori za wataoana kisha baadaye mambo yanakuwa tofauti na kuzidi kuongeza hamu ya mashabiki kuona ni kipi kitafuata ili jambo hilo limalizike waendelee na maisha yao. Kwa kifupi, wameanza kuchoka na drama.
Hata hivyo, kama ulikata tamaa na jambo hilo, stori kubwa mjini kwa sasa ni ndoa ya wawili hao na imewarudisha wengi kwenye kufuatilia nini kitatokea safari hii hasa baada ya Zuchu kumwaga mboga hadharani.
Kama utakumbuka, Zuchu, kupitia ukurasa wake wa Instagram aliandika wameachana kwa sababu hakuna heshima aliyotamani akaipata na alifikia hatua hadi ya kuandika kuishtaki Redio ya Wasafi kupitia kipindi cha Mitikisiko ya Pwani kwa kutotendewa haki na amekuwa akizungumziwa kila wakati kwa mambo mabaya juu yake.

Hakuishia hapo tu, Zuchu pia aliondoa hadi usajili wa lebo ya wasafi kwenye akaunti yake ya Instagram na hapo kila mmoja aliamini ndio basi tena wawili hai sinema limeisha.
Sasa kabla ya wengi walivyotarajia kutokea, nyota wa Bongo Fleva anayefanya vizuri kimataifa Diamond ni kama amefuta mambo hayo baada ya kuibuka na Zuchu kwenye ndoa ya Juma Jux na amedai bado wanatamba mjini.

Ilikuaje?
Katika kuwaaminisha mashabiki hana tatizo na Zuchu, Mondi aliingia naye kwenye sherehe hiyo ya ndoa wakiwa wameshikana mikono huku wakiwa na wapambe 10 nyuma yao.
Katika usiku huo uliokuwa na ndoa hiyo ya kimya kimya, Mondi alitumia muda mwingi kuwa na Zuchu huku wakijipiga picha na kuchukua video fupi wakipigana mabusu muda wote na kucheza kwa kubambiana kwa pamoja.
Mwanaspoti lilikuwa sehemu ya tukio na lilibahatika kwa sukunde kadhaa kuongea na Diamond kuhusu tamko la Zuchu kuachana na alisema yuko naye na bado anatamba naye.

"Hapa si unaona nipo na Zuhura jamani (anacheka) nipo naye na ninatamba naye, ndiyo uwaambie watu hasira za mapenzi watu wasiziingilie, sisi tunaenjoy (akambusu Zuchu)," alisema Diamond, huku Zuchu akiwa anacheka.