MAPENZI: Wenye hekima huwa hawasusi, hutafuta tiba
Muktasari:
- Katika maisha hakuna jambo dogo wala kubwa, hata kama mtu amekwenda kufanya ngono nje,
KAMA unahisi utakuwa kwenye uhusiano ambao hautakuwa na kukwazana, hilo ni jambo unalopaswa kuachana nalo.
Kuna watu wamekuwa na mazoea makubwa ya kununa, yaani akikwazana kidogo tu na mwenzake, anachokiona cha maana kwake ni kununa.
Kwa mfano, anaweza asizungumze kutwa nzima, wiki nzima akidhani huo ni uamuzi wa maana. Kwa kweli tabia hiyo inaudhi.
Kwa ujumla tabia hiyo ambayo wengi wanaiendekeza, ni mbaya na ni lazima wabadilike kama kweli wanapenda maisha yenye furaha katika mapenzi.
Mtu unaweza kununiwa hata mwezi mzima, mpaka ukahisi labda uhusiano umekufa. Wengine hununiwa hadi wanaamua kuwa na uhusiano na mtu mwingine kwa kudhani kule kwingine basi tena, ghafla anamkuta yule aliyenuna anarudi.
Wengine huwa wanarudi na maneno mengi, utamsikia akisema: “Ah unajua siku ile uliniita mjinga uliniudhi sana ulinituhumu nina mtu mwingine ulinikera sana.”
Inatia kinyaa kidogo, hasa mnunaji anapokuwa mama au baba mtu mzima, kuna wale wanaonuna hadi analala kwenye makochi sebuleni!
Swali ninaouliza hapa hivi kuna wanawake ambao hawanuni wala kususa? Wapo wengi tu.
Kuna wanawake wengi wenye hekima huwa hawanuni ovyo.
Ni kwamba wao wanajua katika maisha suala la kukwaruzana lipo, linapotokea cha msingi ni kukaa chini na kuzungumza.
Wengi wanafikiri wanawake ndio wanaoongoza, lakini katika hali ya kawaida ni kwamba kuna kundi kubwa la wanaume nao wamekuwa wakijiingiza katika tabia hizo za kununa ovyo.
Kwa ujumla tabia hiyo si ya watu wa kundi moja tu, bali ni kwa wote, bila kujali umri wao bado wanaendelea na tabia hii mbovu. Tena mara nyingi yule anayenuniwa huwa hajui hata sababu.
Ukiona umenuniwa fahamu kwamba mawasiliano yenu ni hasi sana. Ni ama wewe hujui namna ya kumwingia au yeye haingiliki, hapa nazungumzia mawasiliano. Tatizo kuna wanaojiona kuwa ni wajuaji zaidi ya wengine.
Kuna jamaa mmoja anasema: “Ninapokasirika naweza nikabadilika, nikawa sifurahii kuwa karibu na huyo aliyenikasirisha. Ila huwa sishindwi kumwambia mtu ukweli kuwa amenikwaza.”
Wengine katika kununa kwao huwa na majibu ya mkato. Lakini wengine wananuna kwa sababu ya kuhisi mabaya juu yako labda anahisi umetoka kwenda kwa wapenzi wengine, badala ya kuuliza ambiwe ananuna, yaani wengi hununa kwa kuhisi tu jambo.
MAWASILIANO MUHIMU:
Ili mawasiliano yawepo ni lazima mtu azungumze na si kununa. Kwa ujumla tabia hii ya kununa, siku zote huwa haijengi, bali inabomoa uhusiano. Wakati mwingine katika maisha ya ndoa, ni suala la msingi kushuka ili kupisha mambo mabaya yasije kutokea.
Ndivyo wanavyofanya wanaopendana kwa dhati. Ndugu yangu hitilafu katika uhusiano ni vitu vya kawaida, ni suala la msingi sana kuangalia namna ya kwenda mbele kuliko kuendekeza migogoro.
Kimsingi tabia ya kununa ni upuuzi. Mwenye akili timamu hawezi kukubali kuendelea kukaa na kitu moyoni mwake, hata kiafya hilo ni jambo la hatari, linasababisha mzunguko wa damu kutokuwa wa kawaida.
Ukinuna unasababisha damu kwenda kasi au kwenda pole pole. Haya mambo ya kununa, baadaye katika hali ya uzee wengine huwaletea wengine matatizo ya shinikizo la damu. Kama mtu amekukwaza, zungumza naye mara moja yaishe.
Katika maisha hakuna jambo dogo wala kubwa, hata kama mtu amekwenda kufanya ngono nje, japo si kitu kizuri, lakini unaweza ukamsamehe. Ila ni baada ya kuzungumza.
Ndugu ukifanya hivi unaweza kumbadilisha kabisa mtu wako na mkaishi maisha ya furaha.
Dismas Lyassa ni mtaalamu wa uhusiano kupitia taasisi ya Global Source Watch (GSW), 0653777700