Mziki wa Ngoma, Chirwa wamkuna Naldo Azam FC

Muktasari:

Kabla ya kuanza kutamba kwenye Ligi Kuu, Idd Seleman 'Naldo', alijipatia umaarufu mkubwa kwenye michuano ya Ndondo Cup ndipo Mbeya City ikambeba na msimu huu Azam kumnyakua akiwa ameshaifungia mabao mawili mpaka sasa katika ligi.

MSHAMBULIAJI wa Azam FC, Idd Seleman 'Nado' amekiri viwango bora vilivyoonyeshwa na Obrey Chirwa na Donald Ngoma kwenye mchezo wao wa usiku wa jana umechangia ushindi wa 2-1 walioupata dhidi ya Biashara United katika Ligi Kuu Bara.
Azam ilipata ushindi huo kwenye Uwanja wao wa nyumbani wa Azam Complex kupitia mabao ya Naldo na Nicholas Wadada, huku lile la kufutia machozi la Biashara lilifungwa na Innocent Edwin.
Akizungumza na Mwanaspoti, Naldoalisema safu yao ya ushambuliaji ilicheza kwa muunganiko mzuri na ndio maana ilifanikiwa kupata bao la kuongoza dakika za mapema huku akiweka wazi kuwa wangeongeza umakini zaidi wangeweza kuibuka na ushindi wa mabao mengi zaidi.
"Tulikuwa tunaelewana vizuri kila aliye katika nafasi mbaya ya kufunga alikuwa anahakikisha anampasia aliye katika nafasi nzuri ya kufunga mfano ni bao nililofunga mimi Ngoma ndiye aliyepiga krosi Chirwa kutokana na kubanwa na beki akaamua kuniachia nikiwa mwenyewe nikakwamisha mpira nyavuni," alisema mshambuliaji aliyekuwa Mbeya City na kuongeza;
"Umoja tulio uonyesha jana kama tutaendelea hivyo basi tunaweza kuwa na safu ora ya upachikaji wa mabao kwani kila mmoja atatimiza wajibu wake kwa wakati kila anapopata nafasi nzuri ya kufunga kutokana na kutengenezewa njia," alisema.