Yametimia Ajibu ajifunga Simba miaka miwili

Muktasari:

Ajibu alimaliza msimu akiwa na mabao saba na pasi za mwisho 17

Dar es Salaam. Yametimia mshambuliaji Ibrahimu Ajibu ametambulishwa rasmi Simba leo, Jumatano Julai 3, 2019 saa 7:00 mchana akitokea Yanga.

Ajibu amesajili Simba kwa mkataba wa miaka miwili baada ya kuwepo kwa taarifa nyingi pamoja na nyota huyo kukanusha kusajili kwa mabingwa hao.

Taarifa kutoka ndani ya Simba zinasema Ajibu amesaini mkataba huo wenye thamani ya Sh100 milioni baada ya kuachana na Yanga.

Tangu mwisho wa msimu huu taarifa zimekuwa zinasema Ajibu alisaini mkataba wa miaka miwili kuitumikia Simba, baada ya kuachana kuachana na Yanga pamoja na kukataa kujiunga na TP Mazembe ya DR Congo.

Ajibu alichelewa kutambulishwa Simba kwa sababu uongozi wa klabu hiyo ya Msimbazi ilikuwa inasubiri mkataba wake wa kuitumikia Yanga umemalizika Juni 30.

Pamoja na kuachwa katika kikosi cha Tanzania kilichoshiriki Afcon, Misri mshambuliaji Ajibu aliweka rekodi katika Ligi Kuu Bara msimu uliopita baada ya kutegeneza pasi za mabao 17, na kufunga magoli saba (7) akiwa na Yanga.