Salah amwita kijanja De Bruyne Anfield

Muktasari:
- Staa huyo wa Kibelgiji alithibitisha ataachana na Man City mwishoni mwa msimu huu.
MANCHESTER, ENGLAND: KIUNGO wa Manchester City, Kevin De Bruyne ameibua uwezekano wa kujiunga na klabu nyingine ya Ligi Kuu England baada ya kuaga huko Etihad.
Staa huyo wa Kibelgiji alithibitisha ataachana na Man City mwishoni mwa msimu huu.
De Bruyne mwenye umri wa miaka 33 kwa sasa, licha ya kusumbuliwa na maumivu mara nyingi msimu huu, bado kuna kitu anaweza kukifanya ndani ya uwanja baada ya kile alichokifanya Man City kwa miaka 10.
Licha ya mchezaji huyo mwenyewe kukiri kwamba bado kuna kitu anaweza kukifanya, anataka kwenda kuonyesha ubora wake nje ya England. De Bruyne alishaamua ni wapi atakwenda, lakini itakuwa nje ya England.
Arsenal na Aston Villa zote zimetajwa kufikiria uwezekano wa kumchukua mchezaji huyo, wakati mkali wa Liverpool, Mohamed Salah akitania kwamba atakuwa mwenye furaha kumkaribisha De Bruyne kwenda kukipiga Anfield kama anataka kufanya uhamisho wa utata.
“Nataka kumwambia nampongeza kwa maisha yake ya soka,” alisema Salah.
“Amefanya kazi kubwa sana Man City, na alikuwa mchezaji mahiri kwenye ligi. Namtakia kila la heri…na tunayo nafasi kwa ajili yake!”
De Bruyne anaondoka England akiwa ameshinda mataji ya Ligi Kuu England mara sita na kufunga zaidi ya mabao 100 na kiwango kama hicho kwenye upande wa asisti. Ni mshindi mara mbili wa tuzo ya Mchezaji Bora wa Mwaka.
Timu nyingine zinazohusishwa na De Bruyne ni Napoli, huku kukidaiwa kuwa na ofa za kutoka Saudi Arabia na Marekani, hususani klabu ya Inter Miami.