Al-Khelaifi: Tajiri wa PSG aliyetimiza ndoto

Muktasari:
- Katika fainali iliyokosa ladha iliyokuwa ya upande mmoja dhidi ya Inter Milan, PSG ilitwaa ubingwa kirahisi mno kwa ushindi ulioandika historia mpya ya kipigo kizito zaidi tangu michuano hiyo imeanzishwa cha mabao 5-0, na kuzaa shangwe kubwa kwa mashabiki, lakini zaidi kwa rais wao Nasser Al-Khelaifi.
PARIS, UFARANSA: WIKIENDI iliyopita, ulimwengu wa soka ulishuhudia historia ikiandikwa pale jijini Berlin baada ya Paris Saint-Germain kuibuka mabingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya kwa mara ya kwanza katika historia yao.
Katika fainali iliyokosa ladha iliyokuwa ya upande mmoja dhidi ya Inter Milan, PSG ilitwaa ubingwa kirahisi mno kwa ushindi ulioandika historia mpya ya kipigo kizito zaidi tangu michuano hiyo imeanzishwa cha mabao 5-0, na kuzaa shangwe kubwa kwa mashabiki, lakini zaidi kwa rais wao Nasser Al-Khelaifi.
Nasser ambaye ni mtu aliyesimamia mageuzi makubwa ndani ya timu hiyo tangu awe rais mwaka 2011 kupitia Qatar Sports Investments, ushindi huo ulikuwa kilele cha ndoto yake ya muda mrefu kwani licha ya mafanikio ya ndani ya Ufaransa, kubeba taji hilo ilikuwa ni matamanio yake ya muda mrefu.
Leo tumekusogezea, utajiri wake kamili na jinsi anavyoingiza pesa kiasi cha kuibadilisha timu hiyo kuwa shindani hadi kufikia mafanikio yao ya sasa.

ANAPIGAJE PESA
Chanzo kikuu cha utajiri wake ni uwekezaji mkubwa katika sekta ya matangazo ya michezo, klabu za soka na usimamizi wa mali za kifalme kupitia taasisi ya Qatar Investment Fund ambayo ipo chini ya serikali ya kifalme ya Qatar.
Al-Khelaifi ambaye ni mwenyekiti wa Qatar Investment Fund tangu mwaka 2011, kwa sasa ndio anasimamia kampuni ya beIN Media Group ambayo imenunua haki ya matangazo ya mashindano mbalimbali makubwa duniani kama EPL, UEFA Champions League, na Kombe la Dunia.
Kwa mujibu wa ripoti, kampuni hiyo huingiza mapato ya zaidi ya dola 1.5 bilioni kwa mwaka.
Nasser ambaye pia ni rais wa PSG na timu mbalimbali barani Ulaya kupitia kampuni ya Qatar Sports Investment pia anapiga pesa kutokana na faida ambayo inatokana na timu wanazoziendesha.
Tajiri huyu pia amewekeza binafsi katika biashara za ujengaji wa majumba na kuyakodisha ambapo anamiliki mijengo kibao nchini Ufaransa na baadhi huko Qatar.

MIJENGO
Anamiliki nyumba sehemu tatu, ya kwanza ipo kule Doha, Qatar na ina thamani ya dola 50 milioni ambayo ndio kubwa zaidi kuliko zote.
Vilevile ana mjengo wa maana kule Paris, Ufaransa karibu na uwanja wa PSG ambayo ina thamani ya zaidi ya Euro 20 milioni.
Anamiliki nyumba pia jijini, London, England yenye thamani ya zaidi ya Pauni 25 milioni ambayo inasifika kwa ulinzi wa hali ya juu.

MSAADA KWA JAMII
Nasser Al-Khelaifi ni miongoni mwa watu matajiri wa Kiarabu wanaotoa misaada mikubwa kwa jamii kwa njia tofauti.
Ameripotiwa kufadhili shule na programu za elimu kupitia mashirika ya Qatar, amekuwa akitoa misaada ya kuandaa mashindano ya vijana, pia kwenye vituo vya kukuza vipaji.
Alihusika pia katika kusaidia vifaa vya hospitali na ujenzi wa vituo vya afya hasa wakati wa janga la COVID-19.

NDINGA
Bugatti Chiron -Dola 3 milioni
Rolls-Royce Phantom -Dola 600,000
Lamborghini Aventador -Dola 500,000
Bentley Bentayga - Dola 250,000
Ferrari 812 Superfast - Dola 450,000
Mercedes-Maybach S-Class -Dola 300,000

MAISHA NA BATA
Nasser ana familia, lakini hajawahi kuiweka hadharani ikiwa ni sehemu ya maadili ya Waarabu waliowengi ila ameoa na ana watoto.
Taarifa zinaeleza familia yake inaishi Doha, Qatar na jijini Paris.