Yondani, Abdul kupewa heshima Yanga

Muktasari:

Kelvin Yondani na Juma Abdul ni miongoni mwa wachezaji wakongwe katika kikosi cha Yanga.

UONGOZI wa Yanga baada ya kuachana na baadhi ya nyota wao 14, wamepanga kuwapa heshima wachezaji wao wakongwe Juma Abdul na Kelvin Yondani kama tu watashindwana katika kuendelea msimu ujao na kikosi hiko.

Akizungumza na Mwanaspoti, Afisa Habari wa klabu hiyo, Hassan Bumbuli alisema wachezaji hao ni kati ya wale ambao wamemaliza mikataba yao.

"Bado tunaendelea na mazungumzo nao, hawa ni wachezaji wetu wakongwe kwahiyo lazima tuangalie namna ya kuachana nao kwa heshima," alisema.

"Hatuwezi kusema tumeachana nao wakati hatujamaliza nao mazungumzo, tunaamini kwamba wao wapo tayari kuichezea Yanga pia," alisema.

Aliongeza kwa kusema maamuzi ya wachezaji hao kuendelea kuwa nao katika kikosi kwaajili ya msimu ujao yatatangazwa baada ya kuafikiana.