Yanga yaiteka Mkwakwani

Ukifika sasa Uwanja wa Mkwakwani kama wewe ni shabiki wa wenyeji Coastal UnionĀ  unaweza kuingia ubaridi kutokana na kufurika kwa mashabiki wa wageni wao Yanga.

Mashabiki wa Yanga wameuzingira Uwanja wa Mkwakwani hususan eneo la mbele la lango kuu la kuingia Uwanja huo.

Yanga wanaonekana kuja kwa wingi kuipa nguvu timu yao wakiwa na imani kwamba wanakuja kupindua meza kwa wenyeji wao ambao wamekuwa wakiwasumbua katika Uwanja huu.

Mashabiki hao wametoka mikoa mbalimbali ya karibu kuja kuipa nguvu timu yao katika mchezo huu wa Ligi Kuu Tanzania Bara.

Hata hivyo mashabiki wa Coastal Union hawaonekani kuwa wengi kwasasa eneo hili la Uwanja lakini kikubwa wamekuwa wakiwachimba mkwara wenzao wa Yanga wakiwaambia 'mnatujua tunawachapa tena'.

Coastal Union wamekuwa na rekodi nzuri nyumbani dhidi ya Yanga hali ambayo inawatisha wageni wakijua kwamba mchezo utakuwa mgumu.

Tayari mageti yameshafunguliwa kuanzia saa sita mchana na misururu ya waliokata tiketi imeanza kuingia Uwanjani.