Yanga yaibuka mkutanoni, Simba yasikilizia

Muktasari:
- Simba itakuwa mgeni wa Yanga kwenye mchezo huo wa kiporo wa Ligi Kuu Bara utakaopigwa katika Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam kuanzia saa 11 jioni.
Wakati mechi ya Dabi ya Kariakoo ikitarajiwa kupigwa kesho, Yanga imefanya mkutano na waandishi wa habari, huku Simba iliyotakiwa kufika kwenye mkutano haikutokea.
Simba itakuwa mgeni wa Yanga kwenye mchezo huo wa kiporo wa Ligi Kuu Bara utakaopigwa katika Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam kuanzia saa 11 jioni.
Kabla ya mchezo huo timu hizo mbili zilitakiwa kufanya mkutano wa kikanuni wa wanahabari ambao makocha na manahodha hutakiwa kuhudhuria.
Mapema Yanga ilifika katika ofisi za mdhamini wa ligi ulikotakiwa kufanyika mkutano huo, ambapo kocha Hamdi Miloud na nahodha Dickson Job walifika saa 4:50 asubuhi.
Hamdi na nahodha wake walitangulia kufanya mkutano huo na wanahabari na kumaliza saa 5:18 asubuhi kisha wakaondoka, lakini Simba iliyotakiwa kufuata ambapo mkutano ulitakiwa kuanza saa 5:30 asubuhi, lakini mpaka saa 5:43 ilikuwa haijatokea eneo la tukio.
Baada ya Simba kushindwa kutokea Ofisa Habari wa Bodi ya Ligi Tanzania (TPLB), Karim Boimanda amefunga mkutano huo akisema ratiba zingine zitaendelea.
"Tumejitahidi kuwatafuta Simba, lakini wameshindwa kupatikana. Kwa hiyo ratiba itabidi ziendelee huu ulikuwa ni mkutano wa kikanuni na hili lililotokea litaamuliwa kikanuni," amesema Boimanda.
Juhudi za kujua kwanini Simba haijahudhuria mkutano huo zimeshindwa kufanikiwa kwani Mwanaspoti haijawapata viongozi wa klabu hiyo, kwani hata simu zao zimeita bila mafanikio.
Mchezo huo wa dabi uliahirishwa na Bodi ya Ligi kupigwa Machi 8 na Juni 15, mwaka huu, ambapo ulisogezwa hadi Juni 25.