Ruto aruka tena stori ya viwanja tisa

Muktasari:

Kwenye mahojiano ya hivi majuzi aliyofanya Ruto na runinga ya NTV, alipoulizwa kuhusu ahadi ya viwanja hivyo 11, aliruka stori tena kwa kusema ahadi hiyo haikuwa yake ila ya serikali ya chama tawala Jubilee.

NAIBU Rais William Ruto ameruka stori kuhusu ahadi aliyotoa serikali ya Jubilee itajenga viwanja tisa vya kisasa kufikia 2022.

Ahadi hiyo ilitolewa 2013 na kwenye hotuba ya manifesto ua Jubilee akiwa na Rais Uhuru Kenyatta, Ruto alitamka wazi wazi watajenga viwanja hivyo.

Hata hivyo, mpaka leo hata ujenzi wa uwanja mmoja imekuwa ishu. 2017 Ruto alipohojiwa kuhusu viwanja hivyo, aligeuza tena Kiswahili na kusema serikali imeamua kujenga viwanja 11 badala ya tisa vya awali ilivyokuwa imeahidi.

Kwenye mahojiano ya hivi majuzi aliyofanya Ruto na runinga ya NTV, alipoulizwa kuhusu ahadi ya viwanja hivyo 11, aliruka stori tena kwa kusema ahadi hiyo haikuwa yake ila ya serikali ya chama tawala Jubilee.

Alikwenda hatua zaidi na kusema fedha zilizopaswa kutumiwa kwa ujenzi wa viwanja hivyo, ilitumika kwenye miradi mingine ya serikali.

“Jamani sio kwamba nilikuwa nitoe hela zangu kwa ajili ya ujenzi wa viwanja hivyo, huo ulikuwa mpango wa serikali ya Jubilee wala sio kibinfasi,” Ruto aliruka stori.

Alipohojiwa ikiwa ahadi hiyo ilikuwa tu ya uwongo na njia ya kuomba kura, Ruto alicharuka na kujitetea kwa kusema japo hilo halikufanyika, miradi mingine ilikuwa imefanyika na yote ikiwa ni kwa faida ya wananchi.

“Lakini hivi kwa nini kila leo wanahabari mnashinda mkinisisitizia hili suala la viwanja ni kama ndio mradi wa pekee tulioahidi. Hivi ina maana hamwoni miradi mingine tuliyotekeleza? Akacharuka.