Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Pacome, Aziz KI watoa msimamo Yanga

Muktasari:

  • Aziz KI kwa sasa yupo Afrika Kusini na kikosi hicho ambacho keshokutwa Jumatano kitashuka tena uwanjani kuvaana na TS Galaxy  katika mechi ya pili ya Kombe la Mpumalanga, baada ya juzi kulala 2-1 mbele ya FC Augsburg ya Ujerumani, lakini Pacome yupo kwao Ivory Coast kufuatilia hati ya kusafiria.

VIUNGO washambuliaji wa Yanga, Pacome Zouzoua na Stephane Aziz KI wamezungumza usajili mpya wa kikosi hicho, huku kila mmoja akitoa msimamo wake, lakini wote kwa nyakati tofauti wakiwataja Jean Baleke, Prince Dube na Clatous Chama watakaocheza nao eneo la ushambuliaji la mabingwa hao wa Ligi Kuu Bara.

Aziz KI kwa sasa yupo Afrika Kusini na kikosi hicho ambacho keshokutwa Jumatano kitashuka tena uwanjani kuvaana na TS Galaxy  katika mechi ya pili ya Kombe la Mpumalanga, baada ya juzi kulala 2-1 mbele ya FC Augsburg ya Ujerumani, lakini Pacome yupo kwao Ivory Coast kufuatilia hati ya kusafiria.

Tuanze na Pacome. Nyota huyo amewajibu wale wanaodhani msimu ujao kwa kikosi hicho kutakuwa na vita ya namba baada ya ujio wa kina Chama na wenzake na badala yake alisema mziki umezidi kuimarika.

Akizungumza na Mwanaspoti, Pacome aliyemaliza msimu uliopita na mabao saba alisema hakuna vita yoyote ya namba kama ambavyo wengi wanadhani, lakini sasa kila mchezaji anatakiwa kutumia ubora kuisaidia timu.

Pacome alisema, ujio wa Chama, Dube na Baleke kule mbele utaipa nguvu zaidi timu hiyo ili kuwa na uwiano mzuri zaidi wa kufunga tofauti na msimu uliopita kazi hiyo ilifanywa na viungo washambuliaji zaidi.

"Timu yetu sasa inaweza kuwa na watu wanaoanza  watakaofanya vitu vikubwa na waliobaki nje wakiweka nguvu ili wakiingia kuendeleza walipoanzia wenzao, kifupi mziki umekamilika kwa sasa na tunaamini tutafanya makubwa zaidi ndani na kimataifa," alisema Pacome aliyetua akitokea Asec Mimosas.

"Kikosi sasa kitakuwa na uhakika wa kucheza kwa nguvu na kubadilisha matokeo wakati wowote, kitu kizuri tangu wachezaji wapya wamekuja na kuongeza mzuka kwani sisi tunaishi kama familia na kupeana mikakati ya ushindi."


KUHUSU CHAMA

Akizungumzia kuanza wote watatu kwa maana ya yeye (Pacome), Chama na Aziz Ki, nyota huyo alisema hatarajii sana, japo anaamini kuna mechi wanaweza kucheza hivyo, lakini mwishowe, watakaopata shida ni timu pinzani kwa kuwa wachezaji wote hao ni bora wanajua namna ya kuufungua ukuta wa wapinzani.

"Haiwezekani kutoa silaha zote vitani, ingawa bado jukumu linabaki kwa kocha, lakini ninachoamini ni kwamba, hatutacheza kwa pamoja labda itegemee na aina ya mechi ili kuwepo na sabu imara itakayoendeleza moto dakika 90 za mchezo," alisema Pacome anayetarajiwa kuungana na wenzake wiki hii kambini Sauzi.


AZIZ KI HUYU HAPA

Kwa upande wa Aziz KIm, alisema kuongezwa kwa Chama, Prince Dube na Baleke ni kama kutamrahisishia kazi alizokuwa akizifanya msimu uliopita na wakati mwingine kuigharimu timu.

Yanga mbali na Chama, Dube na Baleke, pia imesajili beki wa kushoto, Chadrack Boka, viungo Duke Abuya na Aziz Andambwile pamoja na kipa Abubakar Khomeiny na Aziz KI anasema mziki huo mpya na wale wa zamani wamezidi kuifanya Yanga kuwa imara zaidi na wapinzani wakae chonjo kwani watachezea sana.

Aziz KI aliyemaliza kama kinara wa mabao wa Ligi Kuu akifunga mabao 21 na kuasisti nane alisema Yanga imefanya usajili mzuri na malengo ya kufanya hivyo ni kuona wanafikia malengo hasa katika Ligi ya Mabingwa Afrika akiamini hata fainali inaweza kufika baada ya msimu uliopita kuishia robo fainali.

"Ni sajili nyingi zimefanyika, lakini nimefurahi kucheza pamoja na Chama, Dube ni wachezaji ambao wameongezeka kikosini kunipunguzia majukumu hasa eneo la ushambuliaji msimu ujao nitakuwa na kazi rahisi japo haina maana kwamba nikipata nafasi sitafunga," alisema Aziz KI na kuongeza;

"Niliposikia Dube anakuja Yanga nilimtabiria ataibuka mfungaji bora sasa imetimia kazi iliyobaki ni kucheza kwa ushirikiano na kumtengenezea nafasi nyingi za kufunga na kwa upande wa Chama nafikiri kila mchezaji anatamani kucheza naye ni mchezaji ambaye anauwezo mkubwa hasa kutoa pasi za mwisho."

Aziz Ki alisisitiza amesalia Yanga ili kuendeleza kazi ya kuipambania timu ifikie mafanikio makubwa ziaid na hasa kuvaa medali za Ligi ya Mabingwa baada ya misimu miwili iliyopita kuvaa za Kombe la Shirikisho.

"Maneno yamekuwa mengi kwamba nimebakizwa na mrembo Hamissa Mobetto sio kweli nimebaki kuipambania Yanga ifikie malengo hilo linawezekana hasa ukiangalia usajili uliofanywa na viongozi kazi imebaki kwetu na benchi la ufundi kuona ni namna gani tunafanya vizuri ndani na nje," alisema Aziz KI na kuongeza;

"Natambua ubora wa kila mchezaji aliyepo kikosini na namna kila mmoja anatamani kuona tunakuwa bora hii inanipa morali ya kuamini kuwa msimu ujao tutakuwa bora zaidi ya msimu uliopita wachezaji waliongezwa wataongeza nguvu na kufanya kile kinachotamaniwa na wengi."