Mwanamuziki wa zamani Adolph Mbinga afariki dunia

Muktasari:
- Mbinga aliyekuwa mpiga solo mahiri amekutwa na umauti saa 5:30 usiku kijijini kwao Mpute Wilaya ya Nachingwea, Lindi.
MWANAMUZIKI Bendi ya Sikinde OG, Adolph Nicholas Mbinga amefariki dunia usiku wa Alhamis jana Juni 15.
Mbinga aliyekuwa mpiga solo mahiri amekutwa na umauti saa 5:30 usiku kijijini kwao Mpute Wilaya ya Nachingwea, Lindi.
Siku za karibuni iliripotiwa kwamba Mbinga aliyekuwa mmoja wa waasisi wa Bendi ya African Stars 'Twanga Pepeta' na aliwahi kupitia katika bendi mbalimbali kama vile Diamond Sound, Mchinga Sound na Mlimani Park 'Sikinde' aliumwa kwa muda mrefu na siku chache hizi za mwisho na ilifikia hatua aliacha kula kabisa.
Mbinga anafahamika kwa utunzi wake mahiri wa Neema akiwa na Diamond Sound na Kisa cha Mpemba akiwa na Twanga Pepeta.
Mpaka sasa taarifa za mazishi yake bado hazijatolewa lakini mipango inapangwa na ndugu, jamaa na marafiki.
Tulimpenda lakini Mungu amempenda zaidi,mwendo ameumaliza, kilichobaki tumuombee mapumziko ya amani.