Mtibwa Sugar yampigia hesabu Baleke

Muktasari:
- Taarifa kutoka katika kambi ya kikosi hicho, zimeliambia Mwanaspoti, Baleke ambaye kwa sasa hana timu tangu alipoachana na Yanga msimu huu, anahitajika kwa ajili ya kuongeza nguvu eneo la ushambuliaji linaloongozwa na nyota, Raizin Hafidh.
BAADA ya Mtibwa Sugar kurejea Ligi Kuu baada ya kushuka msimu uliopita, mabosi wa timu hiyo wako katika mchakato wa kuboresha kikosi hicho, huku wakiwa wanampigia hesabu aliyekuwa mshambuliaji wa Simba na Yanga, Mkongomani Jean Baleke.
Taarifa kutoka katika kambi ya kikosi hicho, zimeliambia Mwanaspoti, Baleke ambaye kwa sasa hana timu tangu alipoachana na Yanga msimu huu, anahitajika kwa ajili ya kuongeza nguvu eneo la ushambuliaji linaloongozwa na nyota, Raizin Hafidh.
Mabosi wa Mtibwa wanahitaji saini ya mshambuliaji huyo ili kutengeneza pacha kali na Raizin ambaye msimu huu wa Ligi ya Championship ameibuka mfungaji bora, baada ya kufunga mabao 18 na kuipatia ubingwa kwa pointi 71.
Licha ya Ofisa Mtendaji Mkuu wa Mtibwa, Swabri Aboubakar kutoweka wazi juu ya dili la nyota huyo, Mwanaspoti linatambua mazungumzo yanaendelea, lakini mchezaji mwenyewe hajafanya uamuzi atacheza wapi msimu ujao.
Mabosi wa Mtibwa wanaamini Baleke anavutiwa na mazingira ya Tanzania, hivyo wanahitaji kumshawishi kumpata.