Mpole afichua siri za Lupopo

Muktasari:

  • Mpole ambaye amerejea nchini, baada ya ligi ya Congo kufutwa msimu huu, alisema kila mchezaji anaishi kwenye nyumba yake, ale nini, afanye starehe ni juu yake mwenyewe, isipokuwa azingatie muda wa mazoezi na aonyeshe kiwango cha juu uwanjani.

STRAIKA wa FC Lupopo, Mtanzania George Mpole amesema jambo kubwa alilojifunza kwenye Ligi Kuu ya nchini Congo ni mchezaji kujisimamia mwenyewe bila uangalizi wa kocha na viongozi, kikubwa kinachotazamwa ni kile anachokitoa uwanjani.

Mpole ambaye amerejea nchini, baada ya ligi ya Congo kufutwa msimu huu, alisema kila mchezaji anaishi kwenye nyumba yake, ale nini, afanye starehe ni juu yake mwenyewe, isipokuwa azingatie muda wa mazoezi na aonyeshe kiwango cha juu uwanjani.

"Wakati najiunga na Lupopo nilikuta ligi imesimama na timu ilikuwa inacheza michuano ya CAF, baadaye ikafutwa hivyo niliambulia kucheza mechi za kirafiki tisa, nilichojifunza wanaamini mchezaji ana akili timamu anapaswa kutambua majukumu yake.

"Hakuna kambi, labda timu iwe inasafiri ndio tunakusanyika pamoja na kufikia hotel moja,sasa ukiwa na akili mbaya unaweza kuona ni uhuru kumbe wanataka ukomae na utambue wewe ni nani kwenye soka, hilo limeniongezea kitu kikubwa sana."

Alisema kuhusu vyakula sahihi kwao, mchezaji mwenyewe anapaswa kutafuta daktari wa kumuelekeza ama kuangalia kwenye mitandao ya kijamii, kipi ale na kipi aache kwa nidhamu ya afya na kazi yake.

Baada ya kurejea nchini, alieleza anatafuta timu ya kufanya nayo mazoezi, kwani kocha wao amewapa programu wanayotakiwa kuifanyia kazi kwa ajili ya kujiandaa na msimu ujao.

"Umebakia mkataba wa mwaka mmoja, kabla ya kuondoka Congo kocha alituachia programu ya mazoezi, nikipata timu yoyote Dar es Salaam nitaanza kuifanyia kazi,"alisema.

Alipoulizwa anaionaje kasi ya washambuliaji wa Ligi Kuu Bara, alijibu; "Sioni atayemfikia Fiston Mayele, maana alikuwa anashindana nao kama Moses Phiri nadhani ni majeraha ndio yaliyowarudisha nyuma, tofauti na msimu wa nyuma ambao tulishinda hadi dakika ya mwisho.