Kipanga yawavimbia Watunisia

Muktasari:
- Timu ya Kipanga ya Zanzibar leo imefanikiwa kutoka suluhu na Club African ya Tunisia katika mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika, mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa Amaan Visiwani humo
BAADA ya kufanikiwa kuvuka raundi ya kwanza ya Kombe la Shirikisho Afrika, timu ya Kipanga imeendelea kuwashangaza wengi baada ya kutoka suluhu na Club African ya Tunisia, mchezo uliopigwa Uwanja wa Amaan Visiwani Zanzibar.
Mchezo huo wa kwanza ulishuhudia upinzani kutoka kwa timu zote huku wenyeji wakionekana kutaka matokeo chanya zaidi ambayo yatarahisisha kibarua chao cha mechi ya marudiano itakayopigwa Oktoba 15 huko Tunisia.
Kipanga ambao ni wawakilishi pekee waliobaki Visiwani Zanzibar kwenye michuano hiyo ilitinga hatua hiyo baada ya kuitoa Al Hilal Wau ya Sudan kwa mikwaju ya penalti 4-3, baada ya mchezo huo kumalizika kwa kufungana bao 1-1.
Matokeo hayo sio mazuri sana kwa kwa Kipanga kwani katika mchezo wa marudiano itahitaji ushindi wa aina yoyote au sare ya kufungana jambo litalowapa manufaa makubwa kwao ya kutinga hatua ya makundi kwa faida ya bao la ugenini.
Hata hivyo haitokuwa mchezo mwepesi kwa Kipanga kwani kikosi hicho cha Africain kinachonolewa na Kocha Mkuu Mfaransa, Bertrand Marchand kina rekodi ya kutwaa Ligi ya Mabingwa Afrika mara moja, ubingwa wa Ligi Kuu nchini mwao mara 13, pia Kombe la Chama cha Soka Tunisia mara 13.