Aussems aendelea na adhabu Simba

Muktasari:

Aussems alisimamishwa na uongozi wa Simba hivi karibuni kutokana na kosa la kuondoka nchini bila kupewa kibali cha mabosi wake.

KOCHA wa Simba, Patrick Aussems ameendelea kutumikia adhabu yake huku kikosi chake kikijifua kwenye Viwanja vya Gymkhana, Dar es Salaam.
Mazoezi hayo yamefanywa chini ya msaidizi wake, Denis Kitambi ambaye alijikita zaidi katika kuwapa wachezaji mazoezi ya kumiliki mpira na kufunga.
Simba ilimsimamisha kocha wake hadi Alhamisi ambapo  itajulikana kama wataendelea naye au la, ingawa habari za chini ni kwamba wameanza mchakato wa kumsaka kocha mpya.
HUKO MAZOEZINI AJIBU NI VITUKO TU
Kwenye mazoezi ya timu hiyo, wachezaji walikuwa wakielekezwa jinsi ya kufunga na ilipofika zamu ya Ibrahim Ajibu kufunga akipigiwa krosi na Yusuph Mlipili, alipiga shuti lililomshinda kipa namba tatu Ally Salim na hapo ndipo alipoanza mbwembwe zake.
Ajibu alianza kumtania Ally akimwambia "Dogo vipi unatishiwa kidogo halafu unaanza kutetemeka yaani mpaka nafunga," kisha akacheka na kuondoka.
Ukiachana na vituko vya Ajibu, Aishi Manula alikuwa akidaka huku akiwakoromea wachezaji akiwatania wanatetemeka nini mpaka wanashindwa kufunga.
"Oya nyie mnatetemeka nini mpaka mnashindwa kufunga, njooni mpige tena msiniogope," kauli ya Manula.
Kocha Kitambi aliwapanga Ajibu, Said Ndemla na Mzamiru Yassin kupiga mashuti ya kufunga huku wapiga krosi akiwa ni Mlipili na Shomary Kapombe.