Anna Bayi kuzikwa Jumamosi nyumbani kwake

Muktasari:
Anna Bayi atakumbukwa kwa akiwa Mwenyekiti Chaneta aliiongoza timu ya taifa (Taifa Queens) kutwaa ubingwa wa Afrika mwaka 2012 na medali ya fedha ya michezo ya Afrika 2011.
Mwili wa Anna Bayi utazikwa Jumamosi Januari 9 kwenye eneo la nyumba yake, Kibaha Mkuza mkoani Pwani.
Mtoto wa marehemu, Sanka Bayi amesema ibada ya mazishi itafanyika kwenye kanisa la KKKT, Mkuza kuanzia saa 5 Asubuhi kabla ya mazishi.
"Mwili kesho Ijumaa utatolewa hospitali kuja nyumbani ambako utalala na jumamosi utapelekwa kanisani kwa ajili ya ibada, kisha utarudi nyumbani kwa ajili ya mazishi ambayo yatafanyika hapa hapa nyumbani,".
Anna Bayi mwenyekiti wa zamani wa Chama cha Netiboli Tanzania (Chaneta) alifariki jana Januari 6, akiwa anapatiwa matibabu kwenye hospital ya Hindu Mandal, Dar es Salaam.
Akisimulia siku za mwisho za Anna Bayi, Filbert Bayi mwanariadha nyota wa zamani na Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC) ambaye ni mme wa marehemu amesema alianza kubanwa na kichomi.
"Alikuwa njiani eneo la Same (Kilimanjaro) anarudi nyumbani, akabanwa na kichomi, oksejeni ikaanza kushuka, kabla ya kupelekwa hospitali ya Sally ambako alitibiwa na kuruhusiwa kurudi nyumbani.
"Hali yake haikuwa nzuri, hapa kwenye kituo chetu cha afya tuna Ambulance, niliwambia wampeleke Hindu Mandal ambako alipelekwa ICU hadi mauti yanamkuta," alisimulia Bayi kwa uchungu.