Wakongwe wapo sokoni Kombe la Dunia 2026
Muktasari:
- Hadi kufikia Julai 2, wachezaji 14 ambao bado wako kwenye Kombe la Dunia hawana mikataba na klabu yoyote. Mashindano yatakapomalizika, hawatakuwa na klabu ya kurejea.
DALLAS, MAREKANI: Kombe la Dunia linaendelea kushika kasi katika hatua za mtoano, njia kuelekea fainali imejulikana, na msisimko unaongezeka kuhusu ni mataifa gani mawili yatakayowania taji kubwa zaidi la soka duniani katika Uwanja wa New York New Jersey tarehe 19 Julai.
Hata hivyo, kwa kundi dogo la wachezaji, kuna motisha nyingine ya kufanya vizuri.
Hadi kufikia Julai 2, wachezaji 14 ambao bado wako kwenye Kombe la Dunia hawana mikataba na klabu yoyote. Mashindano yatakapomalizika, hawatakuwa na klabu ya kurejea.
Miongoni mwao kuna majina makubwa sana, ingawa ni vigumu kuamini kwamba Casemiro, James Rodriguez na Mohamed Salah wana wasiwasi kuhusu hali yao ya kifedha.
Hata hivyo, bado wana nafasi ya kuwavutia waajiri wapya, huku pia kukiwa na hatari ya kupata majeraha kabla ya kusaini mikataba mipya.
BBC Sport imechambua hatma ya muda mfupi ya baadhi ya wachezaji maarufu ambao bado wana ndoto ya kutwaa Kombe la Dunia licha ya kuwa hawana mikataba.
John Stones (Miaka 32, England)
Klabu ya mwisho: Manchester City
Beki Stones ameondoka Manchester City baada ya kuitumikia kwa miaka 10, kipindi ambacho alishinda mataji makubwa 15. Licha ya kusumbuliwa na majeraha hivi karibuni, alichaguliwa na kocha Thomas Tuchel kuichezea England kwenye Kombe la Dunia.
Kwa sasa anahusishwa na uwezekano wa kurejea Everton F.C. au kujiunga na AC Milan.
Casemiro (Miaka 34, Brazil)
Klabu ya mwisho: Manchester United
Manchester United ilimuachia kutokana na mshahara wake mkubwa, licha ya kumaliza msimu wake wa mwisho Old Trafford akiwa katika kiwango bora.
Ameonyesha kiwango kisichokuwa thabiti kwenye Kombe la Dunia, lakini alifunga bao muhimu la kusawazisha katika ushindi wa Brazil dhidi ya Japan baada ya kutokea nyuma.
Anatarajiwa kujiunga na Inter Miami CF mara baada ya mashindano kumalizika.
David Alaba (Miaka 33, Austria)
Klabu ya mwisho: Real Madrid CF
Aliondoka Real Madrid msimu huu wa kiangazi baada ya miaka mitano klabuni hapo.
Nyota huyo wa zamani wa FC Bayern Munich ameshinda mataji 12 ya ligi na mataji manne ya Ligi ya Mabingwa UEFA, huku pia akitajwa kuwa Mchezaji Bora wa Austria mara 10.
Licha ya kuhusishwa na klabu mbalimbali, bado hajatangaza klabu mpya.
Fabinho (Miaka 32, Brazil)
Klabu ya mwisho: Al-Ittihad Club
Kiungo huyo wa zamani wa Liverpool amemaliza mkataba wake nchini Saudi Arabia. Katika mahojiano na Marca mwezi Januari alisema hana haraka ya kuamua hatma yake, lakini anatamani kurejea Ulaya siku zijazo.
Kombe la Dunia limemwona akitokea zaidi benchi chini ya kocha Carlo Ancelotti, lakini bado ni sehemu muhimu ya kikosi cha Brazil.
Mohamed Salah (Miaka 33, Misri)
Klabu ya mwisho: Liverpool.
Miezi yake ya mwisho Liverpool haikuwa rahisi kutokana na kuzorota kwa uhusiano wake na kocha Arne Slot.
Wote wawili sasa wameondoka Liverpool.
Inatarajiwa kwa kiasi kikubwa Salah ataelekea Ligi Kuu ya Saudi Arabia baada ya Kombe la Dunia, lakini kwa sasa ameelekeza nguvu zake zote kuiongoza Misri katika hatua za mtoano.
James Rodriguez (Miaka 34, Colombia)
Klabu ya mwisho: Minnesota United FC
Minnesota United ina chaguo la kuongeza mkataba wake kwa miezi sita hadi mwisho wa mwaka, lakini bado haijafanya hivyo.
Kutokana na kucheza mechi sita pekee katika nusu ya kwanza ya msimu na kuanza kikosi cha kwanza mara mbili tu, haijulikani kama ataendelea kubaki.
Iwapo hatasaini mkataba mpya, Rodriguez anaweza kutafuta klabu yake ya tano ndani ya kipindi kisichozidi miaka mitatu.
Luka Modric (Miaka 40, Croatia)
Klabu ya mwisho: AC Milan
AC Milan ina chaguo la kuongeza mkataba wake kwa mwaka mmoja zaidi, lakini bado haijaamua kama itafanya hivyo.
Haijulikani pia kama Modric ataendelea kucheza sehemu nyingine au atastaafu kabisa.
Alikuwa na kiwango cha chini katika kipigo cha Croatia dhidi ya England hatua ya makundi, lakini alirejea katika kiwango kizuri kwenye ushindi dhidi ya Panama na Ghana, kabla ya kuondolewa katika hatua 32 bora na Ureno.
Orodha kamili ya wachezaji wasio na mikataba ambao bado wapo Kombe la Dunia
David Alaba (Austria) Klabu ya mwisho: Real Madrid
Nabil Bentaleb (Algeria) Klabu ya mwisho: Lille
Casemiro (Brazil) Klabu ya mwisho: Manchester United
Fabinho (Brazil) Klabu ya mwisho: Al-Ittihad
Gideon Mensah (Ghana) Klabu ya mwisho: Auxerre
Thomas Meunier (Ubelgiji) Klabu ya mwisho: Lille
Luka Modric (Croatia) Klabu ya mwisho: AC Milan
Abdul Mumin (Ghana) Klabu ya mwisho: Rayo Vallecano
Orjan Nyland (Norway) Klabu ya mwisho: Sevilla
Th omas Partey (Ghana) Klabu ya mwisho: Villarreal
James Rodriguez (Colombia) Klabu ya mwi sho: Minnesota United
Mohamed Salah (Misri) Klabu ya mwisho: Liverpool
Xaver Schlager (Austria) Klabu ya mwisho: RB Leipzig
John Stones (England) Klabu ya mwisho: Manchester City.