Kufuru... Soka lilivyompa utajiri wa mabilioni Mbwana Samatta

NENDA kusini, kaskazini, magharibu na mashariki, nahodha wa Taifa Stars, Mbwana Samatta ‘Samagoal’ ndiye mchezaji mwenye uwezo mkubwa zaidi kifedha kuliko mchezaji yeyote wa Kitanzania ambaye amevuna mkwanja huo kwenye soka, achana na wale ambao wamekuwa matajiri baada ya kuwekeza kwenye biashara.

Samatta ambaye kwa sasa anacheza soka la kulipwa Ugiriki akiwa na PAOK FC, ameripotiwa kuwa miongoni mwa wachezaji wa Kiafrika ambao wanavuta mkwanja mrefu hiyo ni kwa mujibu wa mtandao wa ERI ambao umekuwa ukifanya tafiti kila mwaka za kina kuhusu viwango vya mishahara vya watumishi mbalimbali katika nyanja tofauti kwa ajili ya haki za mwajiri na mwajiriwa.

ERI imeripoti kiwango cha chini kabisa ambacho mwanasoka anapata huko Ugiriki kama sehemu ya mshahara wake, ni Euro 26.6 kwa saa (Sh. 74, 202) na kwa wachezaji wenye majina makubwa ambao ni kundi la Samatta wanajikusanyia karibu mara nne hadi tano ya kiwango hicho, hapo unaongelea Sh296,808 hadi 371,010 kwa saa.

Kiwango hicho cha fedha ni kwa saa tu na siku moja ina saa 24 hivyo wachezaji wenye majina makubwa kwenye ligi hiyo kwa siku wanakusanya zaidi ya Sh8 milioni (8,904,240) kwa wiki ni zaidi ya Sh62.3 milioni. Hapo unaongelea mshahara na bado bonasi na posho ambazo wachezaji wa PAOK wamekuwa wakipewa kulingana na timu hiyo inavyofanya vizuri. Vigogo hao wiki iliyopita walitinga kibabe kwenye hatua ya robo fainali ya Europa Conference League kwa kupindua meza ya mabao 2-0 ambayo walifungwa ugenini dhidi ya Dinamo Zagreb na wakiwa nyumbani walishinda kwa mabao 5-1.


Kupitia mtandao wake wa kijamii, Samatta alionyesha furaha yake kwa kuweka picha ikimuonyesha akishangilia na wachezaji wenzake kwa kutinga robo fainali huku akiandika maneno yaliyosomeka; “Mazingira ya kustaajabisha, kiwango bora, tupo robo fainali,” alimalizia kwa maneno ya Kigiriki ‘Pame paokara’.

Tukirejea upande wa maokoto, wakati akiwa KRC Genk ya Ubelgiji msimu uliopita ambapo alikuwa kwa mkopo akitokea Fenerbahce ya Uturuki, ilitoka ripoti ambayo ilionyesha Samatta amepata pato la takribani dola 16,513,995 (Sh42.2 bilioni) katika maisha yake ya uchezaji soka barani Ulaya.

Mara ya mwisho alichezea Genk (Ligi Kuu Ubelgiji) msimu wa 2022-2023. Makadirio hayo ni upande wa mishahara tu hayajumuishi bonasi au motisha. Mishahara hiyo sio kiwango halisi walifanya hesabu hizo kulingana na viwango vya fedha ambazo klabu ambazo alikuwa akichezea walikuwa wanalipa kwa wakati huo.

Pamoja na kwamba ni msiri, mipira umemlipa Samatta hakuna ambacho anaudai kutoka kuwa mtoto wa familia ya kawaida tu huko Mbagala ambako yalikuwa makuzi yake hadi kujipata na kujipatia umaa- rufu nchini akiwa na Simba kabla ya kwenda TP Mazembe ya DR Congo hadi Ulaya ambako kumemfanya kuingiza mkwanja mrefu.


Kuna kama Samatta? Hapana, labda kina Kelvin John na Novatus Dismas hapo baadaye kama milango ya kheri itakuwa upande wao maana wamepata bahati ya kuingia Ulaya wakiwa na umri mdogo hivyo wana nafasi kubwa zaidi ya kukusanya maokoto.

Kwa sasa Samatta anachofanya ni kurudisha kwa jamii kulingana na namna ambavyo Mungu alimfungulia milango ya kheri na ndio maana amekuwa na taasisi akishirikiana na rafiki yake, msanii wa muziki wa kizazi kipya, Alikiba iitwayo Samakiba Foundation ambapo kila mwaka huandaa mechi ya hisani kwa ajili ya kusaidia jamii.

Acha hilo, hivi majuzi tu, ulizinduliwa msikiti wa Samatta huko mkoa wa Pwani wenye uwezo wa kuingiza zaidi ya watu 5000.

Unadhani ni nini tena ambacho Samatta mwenye miaka 31 amekabisha zaidi ni kurejesha kwa jamii na kumuomba Mungu amjalie afya njema tu ili awashuhudie vijana wengine wenye damu changa wakivunja rekodi kibao ambazo ameziweka?

Samatta ndiye mchezaji pekee wa Kitanzania ambaye amecheza na kufunga bao kwenye michuano mitatu tofauti ya Ulaya, Ligi ya Mabingwa, Europa League na Europa Conference League, amecheza na kufunga dhidi ya timu kubwa barani Ulaya ikiwemo Manchester City kwenye Uwanja wa Wembley wakati huo akiichezea Aston Villa na Liverpool tena ikiwa nyumbani kwenye uwanja wake wa Anfield.


Tukianza kuongelea yale ambayo ameyafanya Samatta inaweza kutuchukua muda mrefu kuyamaliza, licha ya kuwa pia umri umemtupa mkono lakini bado anaendelea kupambana na yupo kwenye nafasi ya kumaliza msimu akiwa na medali kutokana na PAOK kuwa na nafasi ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Ugiriki.


HIKI KIMEMBEBA

Kati ya vitu ambavyo vimemsaidia Samatta ni kuwa na hofu ya Mungu ndani yake vinginevyo kwa mkwanja ambao amekuwa akikusanya ingekuwa mchezaji mwingine ni rahisi kupoteza mwelekeo, tumeshuhudia hilo kwa wachezaji wengi.

Katika moja ya mahojiano ambayo mchezaji huyo aliwahi kufanya, alisema ukivimba kwa kuonyesha ufahari kwa kile alichonacho unaweza kumuumiza mwingine asiyenacho.