Wimbo wamponza Madee, Basata yamfungia

Baraza la Sanaa la Taifa (Basata) limefungia kujihusisha na muziki, Hamadi Ally “Madee” na kumtaka kushusha mara moja wimbo aliouchapisha jana Desemba 13 wenye maudhui yanayokiuka maadaili.
Taarifa hiyo inasema "Mnamo Desemba 13, 2023 mwanamuziki anayetambulika kwa jina la kisanii ‘Madee’ alichapisha wimbo wenye maudhui yanayokiuka kanuni za Basata za mwaka 2018 na Mwongozo wa kuzingatia maadili katika kazi ya sanaa ya mwaka 2023."
Hivyo basi baada ya kujiridhisha Baraza hilo limemtaka msanii huyo kushusha wimbo huo kwenye mitandao ya kijamii na majukwaa ya kidijitaji na kuufungia kutokuimbwa au kuchezwa mahali popote.
Aidha Baraza limeiomba TCRA kuuzuia wimbo huo kutopigwa kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.
Madee amepigwa faini ya Sh3 milioni kwa kosa hilo na kutofanya shughuli za sanaa hadi atakapolipa faini hiyo.
Na mzalishaji (Producer) wa wimbo huo anayetambulika kwa jina la kisanii Mr T Touch ametozwa faini ya Sh1 milioni sawa na muhusika aliyepandisha wimbo kwenye mitandao ya kijamii na majukumu ya kijiditaji (Digital Platform).