TUONGEE KISHKAJI: Wanaotengeneza filamu, tamthilia Bongo wanajisahau hapa

Tukisema filamu na tamthilia zetu kali sana tutakuwa tumetia chumvi kwa sababu kiukweli bado hatujafikia huko. Lakini pia tukisema filamu na tamthilia zetu mbovu tutakuwa tunawaonea kwa sababu kwenye kuitwa mbovu tumeshavuka, tamthilia nyingi za Bongo zinatazamika siku hizi na filamu ndiyo usiseme, mpaka zinaingia kwenye matamasha makubwa ya kimataifa.

Lakini wakati kazi zao zinakuwa kuna vitu vya maana wanaviacha nyuma, hawavizingatii, hawakui navyo pamoja na kikubwa zaidi ni matangazo.

Watengeneza sinema nchini hawazingatii kabisa kufanya matangazo ya kazi zao wakati kwa wenzetu, nchi zilizotutangulia wana sera ya matangazo ya filamu inayosema, bajeti ya matangazo ya filamu inatakiwa iwe angalau nusu bajeti ya kutengeneza flamu.

Yaani kwa mfano, kama unatengeneza filamu kwa Sh.50 milioni basi hakikisha angalau una bajeti ya kutangaza filamu yako isiyopungua Sh.25 milioni . Na hiyo ni angalau, kuna baadhi ya kampuni za kutengeneza filamu zinakwenda mpaka kufikia asilimia 100 ya bajeti ya matangazo. Yaani bajeti ya kutengeneza ni Sh.50 milioni ya matangazo ni Sh.50 milioni pia.

Huo ni mfano tu, kwa mazingira ya hapa kwetu, kwa sababu ndiyo tupo kwenye hatua za mwanzo za kukuza kiwanda chetu cha filamu sio lazima waandaji watumie sera ya angalau asilimia 50. Wanaweza wakaja na namna yao itawawezesha kutengeneza matangazo ya kueleweka.

Kwa mfano, tangu Alhamisi, muigizaji Vincent Kigosi alikuwa anatangaza tamthilia yake mpya anayopanga kuileta hivi karibuni. Alikuwa anatangaza kupitia Instagram yake na alichokuwa anakiandika ni kwamba; tamthilia hiyo ni bab kubwa kuliko zote tulizowahi kuzitia machoni. Lakini ubaya ni kwamba maneno yake yalikuwa hayaendani na picha anazotuonyesha.

Picha anazoweka zinazoonyesha vitu vya kawaida sana, na hata baadhi ya mashabiki wake kwenye comment waliku wa wanamsanua kwamba mbona picha anazoweka hazionyeshi maajabu.

Vitu kama hivyo wala havihitai bajeti nusu kwa nusu, ni kuamua tu kufanya mambo kitaalamu. Angetafuta mtu maalum wa kumpa jukumu la kumpigia picha za nyuma ya pazia, kisha akatumia picha hiz kufanyia matangazo. Kama wanaona yanawashinda, wanaweza hata kuchota ujuzi kwa wenzao wa Bongofleva, wameiva sana kwenye matangazo. Tunaona wanavyotengeneza makava mazuri ya nyimbo zao, chalenji nzuri kwa ajili ya kazi zao na zaidi.

Lamata Leah anajitahidi sana, amefanikiwa kuifanyia vyema matangazo tamthilia yake ya Jua Kali ukilinganisha na zingine zinaonyeshwa Bongo. Labda alikuwa na bajeti kubwa kuliko au labda ni kujiongeza tu lakini amejitahidi. Alikuwa mpaka na mabango makubwa, amekuwa na ëeventí mbali mbali kuhusu tamthilia yake kama za kutazama episode kwa pamoja, na amekuwa na chalenji kibao za kuhamasisha utazamaji wa kazi yake na imemletea utofauti ó ni kujiongeza tu.