Sarah,  Harmonize ndo basi tena

Sarah,  Harmonize ndo basi tena

Muktasari:

Harmonize kupitia ukurasa wake kwenye mtandao wa Instagram, aliweka picha aliyekuwa  amepiga na mtoto huyo akieleza kuwa ni wa kwake na aliamua kumficha kwa mwaka mmoja na miezi saba kwa kuhofia kuvunjika kwa ndoa yake na Sarah

KAMA ulikuwa unadhani ile ishu ya Harmonize n Sarah juu ya kitendo cha nyota huyo wa muziki wa kizazi kipya kumposti mtoto akidai ni wake imeisha, pole.

Kwani wazi ni hatma ya ndoa ya wawili hao imeshikiliwa na uzi mwembamba baada ya Sarah kutangaza kubwaga manyanga na kutoa ruksa kwa Harmonize kutafuta mwanamke mwingine wa kuishi naye.

Ni hivi. Juzi kati mkali huyo kutoka Konde Gang, alimuanika mtoto anayedai ni wa kwake aliyetajwa kwa jina la Zulekha 'Zuu' na kuibua sintofahamu kwa wawili na sasa imezaa sura mpya zaidi.

Hii ni baada ya mkewe Sarah Michelotti kuzidi kuonyesha hasira kutokubuliana na jambo hilo na kuamua kubwaga manyanga rasmi huku akimtaka kutafuta mwanamke mwingine.

Harmonize ambaye jina lake halisi ni Rajab Abdul na Sara, walifunga ndoa Septemba mwaka jana na kufanya sherehe iliyohudhuriwa na watu wachache wa karibu yao na mpaka leo walikuwa bado hawajajaliwa kupata mtoto.

Hata hivyo, juzi Alhamisi Desemba 4, 2020, Harmonize kupitia ukurasa wake kwenye mtandao wa Instagram, aliweka picha aliyekuwa  amepiga na mtoto huyo akieleza kuwa ni wa kwake na alimaua kumficha kwa mwaka mmoja na miezi saba kwa kuhofia kuvunjika kwa ndoa yake na Sarah.

Kutokanana hilo Sarah naye baada ya saa moja aliweka nyaraka inayoonyesha majibu ya vinasaba (DNA) kwamba mtoto huyo si wa Harmonize ila ameamua kulazimisha.

Hakuishia hapo, kwani jana kupitia tena kwenye ukurasa wa mtandao wa Instagram mwanadada huyo raia wa Italia, alitangaza kumtema rasmi mwimbaji huyo ambapo maelezo yake aliyambatanisha na picha wakiwa katika pozi la kimahaba na Harmonize na kuandika;

"Niliolewa na wewe sababu nilikupenda, ulikuwa kila kitu kwangu na nilikuchagua kama ulivyokuwa na nikakupa mapenzi yangu yote na nilijitahidi kukupa furaha ambayo wewe hukuweza kunipatia.

“ Siku baada ya siku nimekuja kugundua kuwa upo tofauti kabisa na huna adabu kwa mtu yeyote na hukujua kumtunza mwanamke kama mimi au kujivunia kwa mtu ambaye amekupa maisha mazuri na hujui kuheshimu watu waliokupenda na waliokuwa wanakusapoti.

Aliongeza Sarah kwamba muda mwingi amegundua mkali huyo wa wimbo wa Uno kwamba ni ni muongo na bandia kwa kila kitu kwani amepitia mengi kwenye haya mahusiano na kama akiviweka vyote mtandaoni  kila mtu atashangaa sababu ana sura tofauti kabisa  na siku zote anavaa kinyago usoni pake.

“Sina hata maneno mengi yakusema kwa sasa , hujawahi kushukuru hata siku moja kwani niliyokufanyia na sasa umechelewa, maisha yatakufundisha somo ambalo unastahili kwa vitu vyote ulivyonifanyia na kwasasa nitazingatia maisha yangu.

“Ubarikiwe na sasa upo na muda wakuwa na mwanamke yeyote umtakaye njiani, nikushauri jifunze jinsi ya kuthamini na kuheshimu kile watu walichokufanyia,” aliandika Sarah.

Mtoto huyo tayari ameanza kutaradadi katika mitandao ya kijamii akiwa amepigwa picha katika katika mapozi mbalimbali huku mameneja wa msanii huyo kwa nyakati tofauti wakionyesha kumsifia na kumuita majina mbalimbai ikiwemo Kondegirl.