Rich Richie kumbe naye amejipanga

SIKU chache baada ya kuteuliwa kuwa Mjumbe wa Bodi ya Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), mwigizaji Single Mtambalike ‘Rich Richie’ amesema katika utekelezaji wa majukumu yake hataleta ushabiki badala yake ni kuchapa kazi tu.
Richie aliyepokea kwa furaha uteuzi hio na kumshukuru Waziri mwenye dhamana ya sanaa, Dk. Harrison Mwakyembe, alisema kazi aliyopewa ataifanya kwa weledi na si kishabiki kwa vile kuna mambo mengi ya kutekelezwa kwa afya ya sanaa ya Tanzania.
“Nitafanya kazi kulingana na muongozo wa Bodi sawa na wengine, kazi hii inahitaji weledi hivyo sintofanya kishabiki kwa maana ya kutafuta kiki na vitu vingine, naaomba Mungu aniongoze,” alisema Richie.
Moja ya jambo alilopanga kuliangazia kama ni sehemu ya wajumbe wa Bodi ni kuhakikisha anapigania na kutoa elimu ili vijana na jamii nzima ikaacha kulemaa na utandawazi na kurejea katika kuimarisha mila, desturi na tamaduni za Kitanzania kwani ni biashara kubwa ambayo haijatangazwa vya kutosha.