Msama atoa onyo kwa waimbaji

Wakati joto la tamasha la kumshukuru Mungu likizidi kupanda, waandaji wa tamasha hilo wamebainisha kuwa hakuna mwimbaji ataruhusiwa kuimba kwa CD.

Mkurugenzi wa kampuni ya Msama Promotions, Alex Msama amesema katika tamasha hilo wanamuziki wote watatakiwa kuimba live.

Akizungumza na waandishi wa habari amesema katika kufanikisha hilo waimbaji wameingia kambini kufanya mazoezi na bendi.

Msama amesema waimbaji mbalimbali wa muziki wa injili wameendelea kuthibitisha kushiriki kwenye tamasha hilo linalotarajiwa kufanyika  Oktoba 31.

“Waimbaji wanafahamu fika kuwa mwaka huu ni live na watanzania wajiandae kumuona Martha Mwaipaja, Martha Baraka, Rose Muhando na wengine wakiimbia na bendi.

“Hiyo siku licha ya kushukuru na kumuombea Rais wetu tunataka watu waburudike," amesema  na kuongeza.

“Mkumbuke taifa letu limepitia katika mambo mengi sana, kila mtanzania anafahamu kauli mbiu yetu ni 'Tanzania ni nchi yetu,  tuipende, tuilinde' atuna budi kuipenda na kuilinda nchi yetu, tumshukuru Mungu kwa ajili ya taifa letu la Tanzania.” alisisitiza Msama

Aidha Msama amesema baada ya tamasha hilo kufanyika jijini Dar es Salaam, pia litafanyika katika mikoa mingine 10.