Hii ndio sababu ya Linex kuimba kwa hisia

SURA yake imejaa hisia kali kuwasilisha anachomanisha, anapofumbua mdomo wake kuimba mashairi yanayosisimua moyo,  huku akifumba na kufumbua macho kusisitiza umuhimu wa ujumbe wake, hapa namzungumzia msanii wa bongo fleva, Sunday Moshi Mangu 'Linex ' aliywahi kutamba na kibao cha Mama Halima.

Ni miongoni mwa wasanii usioweza  kutilia shaka kusikiliza nyimbo zake mahali popote ama kuangalia video  zake mbele ya mtu yoyote,kutokana na kuzingatia maadili ya Kiafrika, ukiachana na hilo asilimia kubwa ya tungo zake zina visa vinavyoishi na kusisimua.

Linex  hana kiki ila nyimbo zake zina kiki zaidi ya kiki zinazofanywa na baadhi ya  wasanii hapa nchini, wanaokuwa wanatanguliza matukio wakati mwingine yanakuwa ya hovyo ili wazungumziwe ndipo waachie ngoma zao.

Gazeti lako makini la Mwanaspoti limefanya mahojiano maalumu na staa huyo, anafunguka mengi na anaeleza vitu muhimu anavyozingatia katika uandishi wake ili nyimbo yake ikipigwa miaka 10 badae ujumbe uwe unafika kwa mhusika ama kuishi.

"Nipo ndani ya jamii, ninaimba uhalisia wa maisha yanayoendelea kwenye jamii yetu, ndio maana hata nikiimba nakuwa makini kutuliza akili ili ujumbe unapotoka uwe sehemu ya maisha yao, pia napenda zile zinazoishi,  shabiki wangu anayeamua kusikiliza anapata kitu," anasema.


NYIMBO ZAKE ZA HISIA
Anasema kutokana na matukio anayoyaona kila siku kwenye jamii, yanampa umakini wa kukaa chini na kutafakari ni kitu gani anapaswa kukifanya kama kioo cha jamii, hivyo wakati wa kuwasilisha ujumbe anakuwa anaimba kutoka rohoni.

Anasema ndani ya nyimbo zake anaibua tatizo na kuweka ushauri ama kutoa moyo, anakoamini atawafikia wanyonge wanaohitaji faraja ya mtu kuwathamini.

"Mara nyingi ninapokuwa kwenye ari ya kufanya kazi, huwa nazingatia kwamba hawatasikiliza siku moja ama mbili, najua wanakuwa kwenye raha na matatizo, lakini wale wenye matatizo nakuwa nawaletea faraja  ili kuwapa hisia," anasema na anaongeza kuwa;

"Pia inatokana na kulelewa na mama yangu ambaye ni mkulima wa jembe la mkono ambaye alipambana kuhakikisha tunakuwa hadi tulipo, hivyo kila ninachoimba kina maana halisi iwe ndani ya familia ama nje ya familia na huwa simtaji baba mara kwa mara kwasababu sijawahi kuwa karibu na yeye, sijui mengi kumhusu na hajui mengi kunihusu," anasema.


NYIMBO INAYOHUSU MAISHA YAKE
"Wimbo ulionitambulisha kwenye muziki ni Mama Halima ambao ndio ulinitambulisha kwenye muziki, awali wimbo ulikuwa unaitwa Halima lakini uimbaji ndio ukafanya niongeze mama  ili usaundi vizuri, huo una halisia wa maisha yangu ya sanaa, ingawa zote kwangu zina umuhimu mkubwa," anasema.


MUZIKI UMEMLIPA
Anasema muziki ni biashara anapoona inaenda sivyo ndivyo anatuliza akili kujipa muda wa kusoma ramani itakayompa muelekeo wa nini afanye ili umlipe kama anavyotaka na kufichua kwamba ndio sababu ya kukaa kimya kwa muda mrefu bila kutoa ngoma.

"Huwa hainipi hofu kukaa muda mrefu bila kuachia ngoma, kwani najua nina kipaji kikubwa nilichopewa na Mungu, najua nikirudi nakuwa  jambo jipya lakuwafurahisha mashabiki wangu ambao wanapenda kazi zangu," anasema.


ANARUDI KWA KISHINDO
Anasema albamu yake mpya ipo mwishoni kukamilika, anayoielezea itakuwa na  nyimbo za dini zitakazosikilizwa na mtu yoyote kutokana na ujumbe uliomo kwenye nyimbo zake baada ya kukaa kimya kwa muda mrefu.
"Nimefanya hivyo baada ya watu wengi kuniomba nifanye hivyo, kutokana na kusikiliza baadhi ya nyimbo nilizowahi kuziimba za dini kama Kaa Nami, ndio maana albamu inayokuja itakuwa haibagui mtu kwa maana ya mkristo ama muislamu, kijana na mzee,"anasema.

Anasema lengo la kuimba nyimbo za dini sio biashara, badala yake anachukulia kama ibaada ya shukrani kwa Mungu wake, huku akiwakumbusha wasanii wenzake kwamba kazi wanayofanya haimanishi wasiwe wanakwenda mahali patakatifu pakuabudu.

"Narudi kwa kishindo, itakuwa bandika bandua, ukiachana na hizo za dini nina ujio mwingine wa nyimbo za bongo fleva nimeziandaa kwa kutuliza akili, nimezingatia wakati navuma kilikuwa kizazi kingine na hiki ni kizazi kingine, lakini yote hayo sijaenda nje ya maadili yakufanya watu wasiwe huru kuangalia popote," anasema.


TUKIO LA MAUMIVU
Anasema alikuwa na kaka yake mtoto wa mama yake mkubwa alikuwa anaitwa Sunday, ambaye ndiye aliyemkuta kwa mara ya kwanza akiwa amejifungia chumbani kwake anaimba, akiwa hataki mtu amsikie kama ana kipaji, kwani alikuwa hana uhakika wa kuungwa mkono.

"Baada ya kuingia alistajabu sana, nikajua labda ananishangaa kumbe anafurahia aina ya uimbaji wangu, akaniambia niimbe tena nikaimba, ndipo akaniambia niende Dar es Salaam nitatoboa na kufika mbali, nikafanya hivyo, lakini kabla hajaanza hata kula matunda ya kunipambania akaaga dunia, hiyo inaniumiza hadi kesho, tulipendana sana, majina yetu yalikuwa yanafanana, mimi Sunday mdogo yeye mkubwa,"anasema.
Anasema lishamwambia mama yake mzazi kwamba anataka kuwa mwanajeshi, hivyo ikawa inamuwia vigumu kuimba hadharani kwa wakati huo, anasisitiza kwamba hiyo ndoto bado ipo moyoni mwake.


AMTAJA DIAMOND
Anaitaja kolabo  ya nyimbo ya Halima aliyomshirikisha mwanamuziki anayetamba ndani na nje, Diamond Platnumz, kwamba ndio ilikuwa kubwa kutokana na mapokeo kwenye vyombo vya habari na jamii kwa ujumla na kwamba huenda inatokana na nguvu aliyonayo msanii mwenzake.

"Nashukuru vyombo vya habari vilivyousapoti wimbo huo, hata Diamond mwenyewe kukubalia kufanya kazi na mimi, kutokana na hatua aliopo kwasasa ni kubwa ndani na nje ya nchi ana mamilioni ya watu wanaofuatilia muziki wake,  yaani hadi sasa ndio wimbo unaoangaliwa zaidi kwenye mitandao ya kijamii,"


ELIMU YA NDOA
Baadhi ya nyimbo zake  zina ujumbe unaohusu kulinda ndoa, analifafanua hilo kwamba linatokana elimu ya Biblia anayoisoma mara kwa mara tangu akiwa mtoto mdogo, hivyo inampa upana wa kufanya vitu vyenye maana za kuishi katika jamii, inayozisikiliza kazi zake na kuziunga mkono.
Anaeleza hilo baada ya kuulizwa je uimbaji wako unapolenga ndoa kuna changamoto umewahi kukutana nayo kama utakuwa umeoa!!

Anajibu kuwa "Sijao ila nimefanikiwa kupata mtoto mmoja anaelekea kuwa na miaka minne, familia yangu ni mama yangu, mama zangu wadogo, wadogo zangu na  marafiki wa kweli wanaonizunguka," anasema na anaongeza kuwa;

"Kwa sehemu nina ufahamu wa neno la Mungu, nilianza kufundishwa tangu nikiwa mtoto mdogo, najikuta ninakuwa na ujumbe mzito wakati wa kuandika nyimbo zangu, ndio maana nyingine naomba mwisho mwema, kukumbuka ibaada vitu kama hivyo," anasema Linex.