Diamond afunguka kufungiwa kwa Wasafi

Muktasari:

Ikumbukwe kabla ya tukio la kufungiwa, Diamond alikuwa na wastani wa kuchapisha maandiko si chini ya matatu kwa siku kwenye akaunti yake ya Instagram, lakini siku ya jana ilipita patupu.

Dar es Salaam. Hatimaye Mkurugenzi wa Wasafi TV, Naseeb Abdul maarufu Diamond Platnumz ameandika ujumbe wake wa kwanza tangu kituo chake cha runinga kifungiwe kurusha matangazo jana Januari 5 na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).

Diamomd ambaye pia ni muimbaji anayetamba na wimbo wa Waah aliomshirikisha mkongwe Koffi Olomide ameandika ujumbe wake huo kupitia mtandao wa kijamii wa Instagram leo Januari 6 mishale ya saa moja za jioni.

Ikumbukwe kabla ya tukio la kufungiwa, Diamond alikuwa na wastani wa kuchapisha maandiko si chini ya matatu kwa siku kwenye akaunti yake ya Instagram, lakini siku ya jana ilipita patupu.

Ujumbe aliochapisha Diamond leo ikiwa ni zaidi ya masaa 24 yamepita tangu tangazo la kufungiwa unasomeka; "Mwenyezi Mungu amekupa nafasi ili nawe kuwapa wenzio fursa waweze kujikwamua kimaisha… sio kila utakayempa nafasi atakuletea matokeo chanya....Usihuzunike, kubaliana na hilo na uendelee kutoa misaada, kuwapenda na kuwaheshimu wote."

Wasafi TV ilifungiwa kuanzia jana Januari 5, kwa muda wa miezi sita kwa kosa kukiuka kanuni za utangazaji katika matangazo yake ya moja kwa moja ya tamasha la Tumewasha.

Kwa kuanisha zaidi chanzo kilikuwa ni kivazi alichovaa msanii Gigy Money wakati akitumbuiza katika Tamasha hilo.

Gigy Money ambaye ameimba wimbo kama Chombeza na Kiki ni Gigy pia amefungiwa kujihusisha na shuhuli za muziki kwa muda wa miezi sita kwa hilo, adhanu hiyo imetolewa na Baraza la Sanaa Taifa Basata jana.