Bongo tunakwama hapa kupeleka filamu Netflix

Bongo tunakwama hapa kupeleka filamu Netflix

Muktasari:

  • Mtayarishaji wa filamu ya ‘BINTI’ ataja sababu za Tanzania kutoingiza filamu nyingi katika mtandao wa Neflix.

Dar es Salaam. Muongozaji wa filamu ya ‘Binti’ itakayokuwa inapatikana kwenye mtandao wa Netflix, Seko Shamte, ameeleza sababu ya filamu za bongo kutoingia kwenye mtandao huo ikiwa ni pamoja na kukosa wasambazaji.

Soko ameyasema hayo leo Ijumaa Januari 7,2021 wakati alipokuwa akiitambulisha filamu hiyo kwa waandishi wa habari.

Soko alisema hali hiyo inapelekea kuonekana hakuna nafasi ya kuwepo kwa kazi kutoka Tanzania jambo ambalo sio la kweli kwani tatizo kubwa ni kukosekana kwa wasambazaji wa filamu za Tanzania watakaowezesha kufikia katika soko hilo.

Akieleza yeye alivyopenya huko, alisema ni kupitia kampuni ya Media Okada ya nchini Kenya, ambao wamesaini nao mkataba wa kuuza kazi zao.

"Hatuna wasambazaji wa kutoka Tanzania ambao wanapeleka kazi zetu huko japo nilipata nafasi baada ya Media Okada kusaini mkataba wa kuwa wakala wa kazi zetu,”alisema Soko."

Kwa upande wake Katibu Mtendaji Mtendaji Mkuu wa Bodi ya filamu nchini, Dk Kiagho Kilonzo amesema serikalli itaendelea kutoa ushirikiano mzuri kwa wadau wa tasnia ya filamu, kwani ni mwaka 2021 kumefanyika tuzo za filamu kwa mara ya kwanza zenye lengo la kutambua mchango wa Sanaa ya filamu nchini.

Godliver Gordian ambaye ni muhusika mkuu katika flamu hiyo,  alisema mtandao wa Netflix utaweza kuwanufaisha watanzania hususani wasanii wa Bongomovie pamoja na kutangaza utalii uliopo nchini na kuwasihi watayarishaji wa filamu kuwa ipo haja ya kuongeza ubunifu katika kazi za Sanaa kwani kwa sasa mtandao huo utawapa uwanja mpana wa kujitangaza.

‘Binti’ ni filamu inaelezea maisha ya Mama wa kiafrika ambae sio tegemezi, anapambana kwa ajili ya maisha ya watoto wake na familia kwa ujumla.