Basata yamfungia Rosaree miezi sita na faini Sh2 milioni

Muktasari:
Rozaree ana nafasi ya kukata rufaa ndani ya siku 30 kama hajaridhika na adhabu hiyo
Dar es Salaam.Mwanamuziki Rozaree Robert ‘Rozaree’, amefungiwa miezi sita na kupigwa faini ya Sh2 milioni na Baraza la Sanaa la Taifa (Basata) kujihusisha na sanaa kutokana na video ya wimbo wake wa Vitamin U aliyoshirikishwa na msanii kutoka Kenya.
Akizungumza leo Alhamisi Novemba 14, 2019, Kaimu Katibu Mtendaji Basata, Onesmo Kayanda amesema wamefikia hatua hiyo baada ya wimbo huo kukiuka maadili.
Kayanda alisema mwanamuziki huyo amepigwa faini ya Sh 2milioni ambapo kati ya hizo Sh1 milioni ni kwa ajili ya kosa la kukiuka maadili na Sh1 milioni kwa kosa la kwenda kufanya kazi hiyo nchini Kenya bila kibali cha Basata.
"Kilichoonyeshwa katika video ya Vitamin U na msanii wetu Rozaree hakikubaliki katika maadili ya Mtanzania hivyo tumemuita Novemba 6 mwaka huu na kumsomea makosa yake na kamati ya maadili kufikia uamuzi wa kumfungia miezi sita kutojishughulisha na sanaa na kumtoza Sh2 milioni ya faini kwa makosa mawili aliyoyafanya," alisema Kayanda.
Hata hivyo Katibu huyo amefafanua kwamba pamoja na hatua hiyo Rozaree ana nafasi ya kukata rufaa ndani ya siku 30 kama hajaridhika na adhabu hiyo, rufaa ambayo ipo ngazi ya Waziri mwenye dhamana na sanaa.
Pia alitoa wito kwa wasanii kufuata maadili na sheria zilizowekwa katika sanaa ili kuepuka misuguano isiyo ya lazima na serikali.